WHO yakumbwa na hofu kusitishwa ufadhili wa dawa za HIV

 

Shirika la Afya Duniani (WHO) limeonesha wasiwasi mkubwa kuhusu athari za kusitishwa mara moja kwa ufadhili wa programu za HIV katika nchi za kipato cha chini na cha kati.

Programu hizi hutoa ufikiaji wa tiba ya kuokoa maisha ya HIV kwa zaidi ya watu milioni 30 duniani. Takwimu za WHO zinaonyesha watu milioni 39.9 walikuwa wakiishi na virusi vya HIV mwishoni mwa 2023.

Kusitishwa kwa ufadhili wa programu za HIV kunaweza kuwaweka watu wanaoishi na virusi vya HIV katika hatari ya magonjwa na kifo na kudhoofisha juhudi za kuzuia maambukizi katika jamii na nchi.

Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kukabiliana na UKIMWI (PEPFAR), umekuwa mpango mkuu wa mwitikio wa HIV duniani tangu kuanzishwa kwake zaidi ya miaka 20 iliyopita.

WHO imesema kusitishwa kwa sasa kwa ufadhili wa PEPFAR kutakuwa na athari ya moja kwa moja kwa mamilioni ya maisha ambayo yanategemea usambazaji wa matibabu salama na madhubuti ya kurefusha maisha.

PEPFAR inafanya kazi katika nchi zaidi ya 50 duniani kote. Katika miongo miwili iliyopita, ufadhili wa PEPFAR umeokoa maisha ya zaidi ya milioni 26.

Kwa sasa, PEPFAR inatoa matibabu ya HIV kwa zaidi ya watu milioni 20 wanaoishi na virusi vya HIV duniani kote, wakiwemo watoto 566,000 walio chini ya umri wa miaka 15.

Chapisha Maoni

0 Maoni