Ndege nyuki ya Jeshi la Rwanda yaanguka yajeruhi wanafunzi

 

Wanafunzi watatu walijeruhiwa Jumanne baada ya ndege ndogo isiyo na rubani ya Jeshi la Ulinzi la Rwanda (RDF) kuanguka katika Wilaya ya Rutsiro, magharibi mwa Rwanda, kufuatia kupoteza mwelekeo wakati wa mazoezi ya kijeshi kutokana na hali mbaya ya hewa.

Kwa mujibu wa taarifa ya RDF, ndege nyuki hiyo ya kijeshi ilipoteza mwelekeo majira ya saa 7:40 mchana na ikaanguka katika eneo la makazi wakati wanafunzi wakirejea nyumbani kutoka shuleni.

Wanafunzi wawili kati ya watatu waliopata majeraha wanapatiwa matibabu katika Kituo cha Afya cha Kivumu, huku mmoja akihamishiwa katika Hospitali ya Murunda kwa matibabu ya kina.

Katika taarifa yake kwa umma, RDF ilieleza kuwa inaungana na familia za watoto walioumia kwa huzuni na kuahidi kugharamia kikamilifu matibabu yao.

Maafisa wa jeshi wamesema wanaendelea kushirikiana na viongozi wa serikali za mitaa pamoja na wataalamu wa afya ili kuhakikisha watoto wote walioathirika wanapata huduma bora za kitabibu.

"Hili ni tukio la kusikitisha, na tutatoa msaada wote unaohitajika kwa watoto walioumia pamoja na familia zao," ilisomeka sehemu ya taarifa hiyo ya RDF.

Chapisha Maoni

0 Maoni