NCAA yaendelea kuboresha miundombinu ya maji Ngorongoro

 

Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCAA), kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii kwa kushirikiana na Idara ya Huduma za Uhandisi, inaendelea na jitihada za kuimarisha miundombinu ya maji katika vijiji vya Sendui na Irkeepusi, vilivyopo Tarafa ya Ngorongoro, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kuboresha upatikanaji wa huduma hiyo muhimu kwa wanyamapori, mifugo na wakazi wa maeneo hayo.

Tathmini iliyofanywa na wataalamu wa mamlaka hiyo imeainisha maeneo yenye uhitaji wa maboresho, ikiwemo ukarabati wa birika la kunyweshea mifugo katika kijiji cha Sendui, ambalo kwa sasa linahudumia pia vijiji vya jirani vya Alailelai na Bulati.

Aidha, ukaguzi umefanyika katika mradi wa ujenzi wa tanki la maji lenye ujazo wa lita 140,000 lililopo katika Shule ya Sekondari ya Nainokanoka. Tanki hilo limekuwa msaada mkubwa kwa wanafunzi wa shule hiyo pamoja na wakazi wa kijiji cha Irkeepusi na maeneo jirani.

Kwa mujibu wa taarifa ya wataalamu hao, tanki hilo linalenga kuhudumia pia Shule ya Msingi Irkeepusi, lango la Lemala (Lemala Gate) na hoteli mbalimbali zilizopo katika eneo hilo.

Mbali na uboreshaji wa miundombinu, wataalamu wa NCAA kwa kushirikiana na viongozi wa jamii wamekuwa wakitoa elimu ya utunzaji wa vyanzo na miundombinu ya maji kwa wananchi, ili kuhakikisha miradi hiyo inakuwa endelevu na inaleta manufaa kwa muda mrefu.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro imekuwa ikitekeleza miradi ya kijamii kama sehemu ya juhudi za kuhakikisha uhifadhi shirikishi, unaowezesha wananchi kunufaika moja kwa moja na rasilimali zilizopo katika eneo hilo la urithi wa dunia.



Chapisha Maoni

0 Maoni