Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Angellah Kairuki amesema
kuwa Mkutano unaondelea Jijini Arusha utakuwa na manufaa makubwa kwa nchi na
bara la Afrika kutokana na fursa ya majadiliano mahususi ya sekta ya
wanyamapori na misitu hususan biashara ya hewa ukaa.
Akifungua Kikao cha 24 cha Tume ya Misitu na Wanyamapori
Afrika (AFWC 24) na Wiki ya 8 ya Misitu na Wanyamapori Afrika leo, Waziri wa
Utalii na Maliasili, Angelah Kairuki anasema soko la hewa Safi ya Kaboni
lililopo ni fursa muhimu katika kipindi hiki ambacho dunia inapambana kupunguza
athari za hewa ukaa.
Amesema Mkutano huo wa 24 wa kamisheni ya Afrika
inayosimamia Misitu pamoja na wanyamapori kutoka nchi 53 unaondelea Jijini
Arusha kwa siku tano ulianza kufanyika tokea miaka ya 1960 na hii ni takribani
miaka 63 ndio Tanzania inapata fursa ya kufanyika mkutano huo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb)
amesema kuwa, Tanzania imeendelea kuchukua hatua kadhaa za kulinda na kuhifadhi
rasilimali za misitu na wanyamapori kwa ajili ya kusaidia mifumo ikolojia
inayostahimili hali ya maisha pamoja na kuboresha maisha ya wananchi kiuchumi.
“Niwashukuru wajumbe kwa kuchagua Tanzania kuwa mwenyeji na
sisi kama nchi tutaendelea kusisitiza juhudi za uhifadhi na maendeleo chini ya
uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan,” alisema Mhe. Kairuki.
"Kama mnavyojua TFS imeendelea kufanya majadiliano na
wadau katika biashara ya hewa ukaa lakini pia wana misitu, wanaweza kupanda
miti ikatunzwa, ikahifadhiwa bila kukatwa na bado wakalipwa fedha kutoka kwa
wawekezaji duniani wenye mapenzi mema na biashara ya hewa ukaa" anasema.
Kwa upande wa Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za
Misitu Tanzania TFS Prof. Dos Santos Silayo ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa
kwanza wa Kamisheni hiyo amesema kwamba Mkutano huo wa 24 unahudhuriwa na nchi
40 huku ukiwa na mawaziri, wakurugenzi na wadau wa sekta za misitu fursa za
kubadilisha uzoefu katika usimamizi wa rasilimali za misitu na wanyamapori
lakini pia kuweka mikakati ya kukabiliana na changamoto za sekta hizo.
Anataja moja ya changamoto wanayokumbana nayo ni mabadiliko
ya tabianchi ambapo mataifa ya Afrika yanapaswa kuweka mikakati ya pamoja kwa
sababu faida za rasilimali misitu zinavuka mipaka.
Prof. Silayo amesema, lengo la Mkutano huo ni kubadilishana
uzoefu wa pamoja ili waweze kutatua changamoto mbalimbali katika sekta ya
misitu na wanyamapori.
“Hadi sasa tuna washiriki takriban 300, lakini wapo pia
wanaoshiriki kupitia njia ya mtandao. Tunaamini kupitia majadiliano nchi
washiriki zitakwenda kunufaika lakini hasa sisi watanzania, na moja ya
majadiliano tutakayofanya ni juu ya biashara nzima ya hewa ukaa ambayo sasa
kama nchi tunakwenda kunufaika nayo.”
Naye Mwakilishi wa Shirika la Chakula na Kilimo (FAO)
nchini, Dk Nyabenyi Tipo aliipongeza Tanzania kwa kuingiza ajenda ya mazingira
na aliwapa changamoto washiriki waliokusanyika katika mkutano huo kuongoza
mapambano ya kuokoa dunia.
Kamisheni ya Misitu na Wanyamapori ya Afrika ilianzishwa na
Mkutano wa FAO mwaka 1959 na inatoa jukwaa la sera na kiufundi kwa nchi za
kanda ya Afrika kujadili na kushughulikia masuala ya misitu kwa misingi ya
kikanda chini ya kaulimbiu "Usimamizi Endelevu wa Rasilimali za Misitu na
Wanyamapori Afrika, Kukuza Usalama wa Chakula na Ustahimilivu wa Mabadiliko ya
Tabianchi kwa ajili ya kuboresha maisha ya watu”.
0 Maoni