Vifo vya wakina mama wakati wa kujifungua vyapungua kwa 80%

 

Ripoti ya Utafiti wa Afya ya Uzazi, Mtoto na Viashiria vya Malaria Tanzania 2022, inaonesha kuwa vifo vitokanavyo na uzazi kwa wakina mama wakati wa uzazi vimepungua kutoka vifo 530 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2015/16 hadi kufikia vifo 104 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2022.

Takwimu hizi zimetolewa leo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati akizindua ripoti hiyo jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa kwa sasa kiwango cha vifo vya uzazi kwa wakina mama nchini kimepungua kwa asilimia 80.

“Kwangu binafsi kama kiongozi na kama mzazi naijua vyema kazi inayofanyika kule ndani, na kutoka ukiwa hai basi ni baraka ya Mungu, sasa nibaraka ya Mungu lakini ni Serikali kujipanga na vifaa ili matatizo yanapotokea basi uweze kusaidiwa kwa haraka,” alisema Rais Dkt. Samia na kuongea “Na kwa sababu nimesha pita huko kama mzazi na Mhe. Waziri wa Afya Ummy Mwalimu alishapita huko kwahiyo tukasema tufunge kibwebwe tuifanye hii kazi.”

Amesema shabaha ya Malengo ya Maendeleo Endelevu SDGs yanaagiza ifikapo 2030 vifo vitokanavyo na uzazi kwa kina mama wakati wa uzazi visizidi 70 kwa kila vizazi hai 100,000, “Sisi tupo 104, safari yetu mpaka 2030 tunaweza kufikia hayo malengo”.

Rais Dkt. Samia amewataka madaktari na wakunga kutobweteka na mafanikio hayo bali waende wakafanye kazi, kwani vifaa vipo wakafanye kazi kwenda kuokoa uhai wa wakina mama wajawazito nchini.

Pia, ripoti hiyo imeonyesha kupungua kwa idadi ya vifo vya watoto waliochini ya umri wa miaka 5, kutoka vifo 67 kwa kila vizazi hai 1,000 mwaka 2015/16 hadi kufikia vifo vya watoto 43 kwa kila vizazi hai 1,000 mwaka 2022.

“Kwa upande wa watoto wachanga hapa bado kunakazi ya kufanya kwa sababu vimepungua kwa asilimia 1, na inawezekana kabisa hatukuwa na vifaa vya kusaidia kuokoa maisha ya watoto wanaozaliwa,” alisema Dkt. Samia.

Rais Dkt. Samia amesimulia kwamba kunakipindi alienda kumuangalia mjukuu wake aliyezaliwa njiti, alikuta hali ambayo ilimtoa machozi hospitalini kwa mara nyingine tena, hakuna mashine vitoto vimepangwa kwenye mashine moja vinalialia, wengine wamebebwa na mama zao.

“Nilipofika kwa mjukuu wangu nikamuaona amewekwa juu ya meza anapigwa na taa kwa juu nikasema kwamba huyu mbona mumemweka hapa nikaambiwa anapata joto hapa ndio anapata uhai wake,” alisema Dkt. Samia na kuongeza “Nikasema kwamba hii hali hairidhishi leo namshukuru Mwenyezi Mungu ametusaidia tumegawa vifaa 123 vya watoto njiti.”

Pamoja na mambo mengine ripoti hiyo imeonyesha kumekuwepo na mafanikio ya kupungua kiwango cha mimba za utotoni kwa watoto wa kike wenye umri wa kuanzia umri wa miaka 15 hadi 19, kutoka asilimia 27 mwaka 2015/16 hadi asilimia 22 mwaka 2022.

Rais Samia ameitaja mikoa inayoongoza kwa kuwa na kiwango kikubwa cha mimba za utotoni kuwa ni Songwe 45%, Ruvuma 37%, Katavi 34%, Mara 31%, Rukwa 30%. Aidha, katika mikoa ya Dar es Salaam, Njombe na Ruvuma viwango vya mimba za utotoni vimeongezeka.

Chapisha Maoni

0 Maoni