Spika wa Bunge , Dk Tulia Ackson ameteuliwa na Tanzania kuwania Urais wa Umoja wa Mabunge la Dunia (IPU) katika uchaguzi utakaofanyika Oktoba, 2023.
Uteuzi huo, umetangazwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Stergomena Tax baada ya kikao na mabalozi wa nchi mbalimbali kuhusu Tanzania kuwania nafasi hiyo.
Dk Tax amesema nafasi hiyo itaitangaza Tanzania kimataifa na kupata nafasi ya kuyasimamia masuala yenye maslahi ya kidunia.
Uteuzi wa Dk Tulia kuwania nafasi hiyo, umetokana na kile kilichoelezwa na Dk Tax kuwa anastahili kutokana na uwezo na uzoefu alionao kwenye uongozi.
Dk Tulia akichaguliwa atakuwa mwanamke wa kwanza kuliongoza Bunge hilo, lenye nchi wanachama 179 na wabunge 705 wanaoziwakilisha nchi zao.
Historia
Dk Tulia Ackson alizaliwa katika Kijiji cha Bulyaga, wilayani Tukuyu mkoani Mbeya Novemba 23 mwaka 1976. Ni mhitimu wa Shahada ya Uzamivu (PhD) katika sheria
Dk Tulia Ackson kabla ya kuingia katika duru za siasa alikuwa mhadhiri wa Sheria katika Kitivo cha Sheria cha chuo Kikuu cha Dar es Salaam
Februari mwaka 2014, Rais wa awamu ya nne Jakaya Kikwete alimteua kuingia katika Bunge Maalumu la Katiba akiwakilisha Jumuiya na Taasisi za Elimu ya Juu.
Septemba mwaka 2015 Dk Tulia aliteuliwa kuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Novemba mwaka 2015, Rais wa awamu ya tano hayati John Magufuli alimteua kuwa mbunge wa viti maalumu kutoka katika nafasi 10 anazoruhusiwa kikatiba na baadae kuteuliwa kuwa Naibu Spika
Mwaka 2020 alichaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Mbeya mjini na baadaye Spika wa Bunge la Tanzania baada ya kujiuzulu kwa aliyekuwa spika Job Ndugai.
1 Maoni