Wananchi wa Kijiji cha Nsekwa, Kata ya
Nsekwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlele mkoani Katavi wametoa pongezi zao
kwa Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa
kutengeneza barabara za lami Kilomita 3.73 ili kuwezesha shughuli za usafiri na
usafirishaji.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti,
wananchi hao wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha kupata
barabara za lami katika kijiji chao ambazo zimeweza kuwasaidia katika shughuli
zao za kila siku.
Diwani wa Kata ya Nsekwa, Mhe. Elijius
Malando alisema, barabara hizo zimewasaidia wafanyabiashara kufika kijijini
kwao kununua asali, karanga na mahindi ambapo kwa niaba ya wananchi ameishukuru
serikali kwa kujenga barabara inayoanzia makao makuu ya Wilaya kuja kijiji cha
Nsekwa kwani imewasaidia wananchi kuzifikia huduma za kijamii kwa urahisi.
“Wananchi wamefurahi wanasafirisha
bidhaa zao kwa urahisi na biashara zimeongezeka watu wamefungua maduka,
tunamshukuru Rais Samia kwa barabara za lami ambazo zimewakomboa wajawazito waliokuwa
wanajifungulia njiani kwasasa wanafika hospitali ya wilaya kwa urahisi,”
alisema Mhe. Malando.
Naye, Mkazi wa kijiji cha Nsekwa Bw.
Deogratius Nicholaus alisema, hapo awali usafiri ulikuwa shida walikuwa
wanatumia nauli ya pikipiki shilingi 10,000 lakini sasa nauli ni shilingi 5000,
pia walikuwa wanatumia masaa mawili hadi matatu kufika mjini lakini sasa
wanatumia dakika 45 kufika mjini.
“Tunaishukuru serikali kutupatia
barabara sasa tunafanya biashara kwa urahisi, kabla ya lami kulikuwa na
michanga mingi, kutoka kijijini kwenda Inyonga tulikuwa tunatumia masaa mengi
kupeleka wagonjwa na kufuata huduma za kijamii lakini sasa tunapita kwa urahisi,”alisema.
Kwa upande wake, Bi. Anusiata Simon
mkazi wa kijiji cha Nsekwa, ameishukuru serikali kwa kujenga barabara ambazo
zimerahisisha usafiri wa kutoka kijijini kwenda Inyonga hadi Mpanda na amesema
kwasasa wakiagiza bidhaa zinafika kwa wakati na wanafanya biashara hadi usiku
kwa sababu ya taa za barabarani zilizowekwa ambazo zimeongeza usalama na kijiji
kimependeza.
Meneja wa TARURA Wilaya ya Mlele,
Mhandisi Paul Mabaya, ameishukuru serikali kwa kuwapatia fedha takribani
Bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa barabara za lami Km 3.73 ambazo ni barabara
ya Inyonga-Nsekwa Km 2, Mapili-Utene Km1 na Uzega-Kafulu Km 0.73 zilizopo
Kijiji cha Nsekwa katika Halmashauri ya Mlele ambapo barabara ya Utene na
Inyonga mradi umekamilika asilimia 100 upo katika kipindi cha matazamio cha
mwaka mmoja.
Muonekano wa barabara ya lami iliyotengenezwa na Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) katika Kijiji cha Nsekwa, Kata ya Nsekwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlele mkoani Katavi, yenye urefu Kilomita 3.73.
0 Maoni