Kwa mara ya kwanza katika historia, nishati mbadala
imeipita makaa ya mawe kama chanzo kikuu cha umeme duniani katika nusu ya
kwanza ya mwaka huu, kwa mujibu wa takwimu mpya kutoka kwa taasisi ya utafiti
wa nishati ya kimataifa, Ember.
Ingawa mahitaji ya umeme yanaendelea kuongezeka duniani
kote, ongezeko la matumizi ya nishati ya jua na upepo lilikuwa kubwa kiasi cha
kukidhi asilimia 100 ya ongezeko hilo la mahitaji, na hata kuchangia kupungua
kwa matumizi ya makaa ya mawe na gesi asilia kwa kiasi kidogo.
Hata hivyo, Ember inasema mafanikio hayo yanaficha
picha tofauti kimataifa.
Nchi zinazoendelea, hususan China, ndizo
zilizoongoza mapinduzi ya nishati safi, huku mataifa tajiri kama Marekani na
zile za Umoja wa Ulaya (EU) yakiongeza utegemezi wao kwa vyanzo vya nishati
vinavyochangia ongezeko la joto duniani.
Pamoja na mafanikio hayo, makaa ya mawe bado
yalibaki kuwa chanzo kikuu cha uzalishaji wa nishati duniani mwaka 2024, nafasi
ambayo yameshikilia kwa zaidi ya miaka 50, kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa
la Nishati (IEA).
China inaendelea kuongoza kwa kasi katika uwekezaji
wa nishati safi, ikiwa imeongeza uwezo wa kuzalisha umeme kwa kutumia jua na
upepo kuliko jumla ya uwezo ulioongezwa na mataifa yote mengine duniani.
Hatua hiyo imeiwezesha China kuzalisha nishati
mbadala kwa kiwango kikubwa kiasi cha kuzidi ongezeko la mahitaji ya umeme,
hali iliyosaidia kupunguza uzalishaji wake wa nishati inayotokana na mafuta ya
kisukuku kwa asilimia 2.

0 Maoni