MSEMAJI
wa Jeshi la Polisi, David Misime, amesema hali ya usalama nchini
inaendelea kuwa shwari kutokana na ushirikiano mkubwa linaoupata
Jeshi la Polisi kutoka kwa wananchi pamoja na wadau wengine katika
kubaini, kuzuia na kutanzua vitendo vya uhalifu.
Misime
amesema pamoja na hali hiyo ya usalama kuwa nzuri, yapo matukio
machache ya kihalifu yaliyojitokeza katika maeneo mbalimbali nchini
na ambayo yameendelea kushughulikiwa kwa ufanisi mkubwa kwa mujibu wa
sheria.
Amesema Makamanda wa Polisi wa Mikoa na Vikosi
wamekuwa wakitoa taarifa mara kwa mara kuhusu kukamatwa kwa wahalifu
waliotenda uhalifu, kufikishwa kwao mahakamani, na kwa baadhi yao
kupatikana na hatia na kuhukumiwa kwa mujibu wa sheria.
Misime
amesema katika siku za hivi karibuni kumekuwa na maswali kutoka kwa
baadhi ya wananchi kuhusu namna Jeshi la Polisi linavyofuatilia na
kushughulikia vitendo vya uhamasishaji wa uvunjifu wa amani
vinavyoonekana kufanywa na baadhi ya watu kupitia mitandao ya
kijamii.
Amesema Jeshi la Polisi linafuatilia kwa karibu sana
shughuli zote za aina hiyo zinazofanywa na baadhi ya watu ambao awali
walikuwa wakihamasishana kufanya maandamano nchini Julai 7.
Kwa
mujibu wa Misime, kutokana na ufuatiliaji unaofanywa na Jeshi la
Polisi kwa saa 24 kupitia mifumo mbalimbali pamoja na kwenye mitandao
ya kijamii, imebainika kuwa watu hao wameondoka kwenye ajenda ya
kuhamasisha maandamano yasiyozingatia matakwa ya sheria na sasa
wanahamasishana kufanya vitendo vya uhalifu.
Amesema miongoni
mwa vitendo hivyo ni kuhamasisha kufunga barabara, uchomaji moto wa
shule ili kusababisha taharuki kwa wazazi na walezi, kushambulia
wananchi, kukata watu vichwa na kuua baadhi ya watu, pamoja na
kuharibu mali za umma na binafsi.
Misime amesema watu hao pia
wamekwenda mbali zaidi kwa kuhamasishana kupitia majukwaa mbalimbali
ya mitandao ya kijamii kuvamia askari wa vyombo vya ulinzi na usalama
kwa lengo la kuwapora silaha ili kuzitumia kufanya uhalifu
wanaoupanga.
Amesisitiza kuwa uhamasishaji wa uhalifu huo wa
kijinai unaofanywa chini ya kivuli wanachokiita haki ya kufanya
maandamano ya amani haukubaliki kwa sababu ni kinyume na sheria za
nchi, misingi ya utawala wa sheria pamoja na mikataba ya kikanda na
kimataifa na ni hatari kwa usalama wa nchi.
Misime amesema
hakuna haki ya kuhamasisha kufanya vitendo vya kihalifu
vinavyokusudia kuhatarisha usalama wa maisha ya watu na mali zao na
vinavyokiuka haki za watu wengine kwa kuwajengea hofu kila siku na
kutaka kuwanyima uhuru wao wa kufanya shughuli zao za kila siku za
kujitafutia kipato.
Ameeleza kuwa Jeshi la Polisi linaendelea
kuchukua hatua stahiki dhidi ya watu wote wanaojihusisha na vitendo
hivyo na linaendelea kuwafuatilia kwa karibu sana kwa mujibu wa
sheria za nchi.
Aidha, ametoa wito kwa wananchi kuendelea
kushirikiana katika kukataa na kupinga vitendo vyote vya kihalifu
vinavyolenga kuhatarisha maisha ya wananchi, mali zao, mali za umma
na amani ya nchi.
Pia ameshauri mtu yeyote anayepokea ujumbe
unaohamasisha uhalifu wa aina hiyo kutousambaza, bali kuufuta na
kutoa taarifa kwa vyombo husika ili kuchukua hatua.
Misime
amesema Jeshi la Polisi linawahakikishia wananchi kuwa hali ya
usalama nchini itaendelea kuwa shwari, yenye amani, utulivu na
usalama kutokana na ushirikiano wa karibu kati ya Jeshi la Polisi
pamoja na vyombo vingine vya ulinzi na usalama.

0 Maoni