Zaidi ya ekari kadhaa za bangi zimeharibiwa katika operesheni
maalumu iliyofanyika ndani ya Hifadhi ya Msitu wa Ukwiva, wilayani Kilosa,
mkoani Morogoro, ikihusisha ushirikiano wa vyombo vya ulinzi na usalama pamoja
na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).
Operesheni hiyo, iliyofanyika Septemba 26, ilihusisha timu kutoka
Ofisi ya DSO, Jeshi la Polisi kupitia Ofisi ya OCD, wawakilishi wa Ofisi ya
DAS, kikosi cha Mgambo na watumishi wa TFS. Mashamba ya bangi yaliyokutwa ndani
ya hifadhi hiyo yaliteketezwa mara moja.
Akizungumza baada ya zoezi hilo, Kiongozi wa Operesheni hiyo SSP
Janeth D. Nganda Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kilosa (OCD) alisema: “Tunatoa onyo
kali kwa wananchi wote wanaojihusisha na kilimo haramu ndani ya misitu ya
hifadhi. Serikali haitavumilia vitendo vya aina hii vinavyohatarisha usalama wa
hifadhi na mustakabali wa rasilimali za taifa.”
Kwa mujibu wa Kamanda wa Kanda ya Mashariki wa TFS, PCO Mathew
Ntilicha lengo la doria hiyo lilikuwa kuimarisha ulinzi wa hifadhi na kuzuia
misitu kubadilishwa kuwa mashamba ya kilimo haramu, ikiwemo bangi.
Aidha, operesheni hiyo pia ililenga kutoa elimu na kuhamasisha
wananchi kuepuka uharibifu wa mazingira.
Aliongeza kuwa misitu ya hifadhi ni mali ya taifa na inapaswa
kulindwa kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho na kuongeza kuwa operesheni za
aina hii zitaendelea katika maeneo
mbalimbali ya hifadhi nchini, ili kuhakikisha usalama wa misitu na kupunguza vitendo
vya uhalifu wa mazingira.




0 Maoni