Doria yaangamiza mashamba ya bangi Ukwiva

 

Zaidi ya ekari kadhaa za bangi zimeharibiwa katika operesheni maalumu iliyofanyika ndani ya Hifadhi ya Msitu wa Ukwiva, wilayani Kilosa, mkoani Morogoro, ikihusisha ushirikiano wa vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).

Operesheni hiyo, iliyofanyika Septemba 26, ilihusisha timu kutoka Ofisi ya DSO, Jeshi la Polisi kupitia Ofisi ya OCD, wawakilishi wa Ofisi ya DAS, kikosi cha Mgambo na watumishi wa TFS. Mashamba ya bangi yaliyokutwa ndani ya hifadhi hiyo yaliteketezwa mara moja.

Akizungumza baada ya zoezi hilo, Kiongozi wa Operesheni hiyo SSP Janeth D. Nganda Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kilosa (OCD) alisema: “Tunatoa onyo kali kwa wananchi wote wanaojihusisha na kilimo haramu ndani ya misitu ya hifadhi. Serikali haitavumilia vitendo vya aina hii vinavyohatarisha usalama wa hifadhi na mustakabali wa rasilimali za taifa.”

Kwa mujibu wa Kamanda wa Kanda ya Mashariki wa TFS, PCO Mathew Ntilicha lengo la doria hiyo lilikuwa kuimarisha ulinzi wa hifadhi na kuzuia misitu kubadilishwa kuwa mashamba ya kilimo haramu, ikiwemo bangi.

Aidha, operesheni hiyo pia ililenga kutoa elimu na kuhamasisha wananchi kuepuka uharibifu wa mazingira.

Aliongeza kuwa misitu ya hifadhi ni mali ya taifa na inapaswa kulindwa kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho na kuongeza kuwa operesheni za aina hii  zitaendelea katika maeneo mbalimbali ya hifadhi nchini, ili kuhakikisha usalama wa misitu na kupunguza vitendo vya uhalifu wa mazingira.




Chapisha Maoni

0 Maoni