MCT, Uwezo Tanzania waungana kimarisha uandishi wa habari za elimu

 

Baraza la Habari Tanzania (MCT) na Uwezo Tanzania wametia saini makubaliano ya ushirikiano wa miaka mitatu yenye lengo la kuimarisha uandishi wa habari za elimu nchini, kuhamasisha ushiriki wa jamii katika masuala ya elimu, na kukuza matumizi ya tafiti na ushahidi katika kuripoti stadi za maisha na maendeleo ya kujifunza kwa watoto.

Makubaliano haya muhimu, yaliyosainiwa leo tarehe 01 Oktoba, 2025, kati ya  Katibu Mtendaji wa MCT, Ernest S. Sungura, na Mkurugenzi Mtendaji wa Uwezo Tanzania, Baraka Mgohamwende, ambao utekelezaji wake unaanza mara moja yamelenga kuwajengea waandishi wa habari uwezo wa kuandika habari zenye kina kimaudhui, usahihi, na mvuto ili kuchochea mijadala ya kitaifa na kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Akizungumza kabla ya utiaji saini Sungura alisema kwamba kupitia ushirikiano huo, waandishi wa habari wanatarajiwa kunufaika na fursa mbalimbali, ikiwemo,mafunzo ya kitaaluma na programu za kukuza uwezo wa uhariri.

Fursa zingine ni upatikanaji wa takwimu sahihi na ripoti za utafiti za elimu,kupata ruzuku kwa waandishi wa habari za elimu na kuendeleza kuendeleza Tuzo ya uandishi wa habari za elimu kupitia Tuzo za Umahiri katika Uandishi wa Habari Tanzania (EJAT) zinazoratibiwa na MCT.

MCT ilieleza pia  Makubaliano hayo yanatilia mkazo uandishi jumuishi kwa kuhakikisha sauti za wasichana, makundi yaliyotengwa, na wanafunzi walioko katika mazingira hatarishi zinatambuliwa na kupewa nafasi katika vyombo vya habari.

Baraza la Habari Tanzania, kupitia kitengo chake cha ushauri wa kitaaluma (MICS), kitaratibu utekelezaji wa makubaliano haya, huku kikishirikisha vyombo vya habari na waandishi huru. Pia, Baraza litatoa majukwaa ya kusambaza tafiti za Uwezo Tanzania na washirika wake kwa umma.

Kwa upande wa Uwezo Tanzania, Mkurugenzi wake, Baraka amesema shirika hilo lililojikita katika tathmini za kijamii za kujifunza na kuhamasisha sera za elimu, kutokana na makubaliano hayo watahakikisha wanawawezesha waandishi wa habari kuandika habari za elimu kwa weledi, kwa kutumia ushahidi, na kwa kuzingatia usawa wa kijinsia.

Alisema dhamira ya ushirikiano huo ni kuhakikisha kuna taarifa za kutosha za ushawishi ili kila mtoto apate fursa ya kujifunza kwa ufanisi na kujengewa uwezo wa kukabiliana na changamoto za maisha kupitia program za stadi mbalimbali za maisha zinazowezeshwa na  Uwezo Tanzania.

Washirika wengine katika utekelezaji wa mradi huu wa stadi za maisha na maadili ni pamoja na Organization for Community Development (OCODE), Milele Zanzibar Foundation (MZF), na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (University of Dar es Salaam).





Chapisha Maoni

0 Maoni