Mwanamke ahukumiwa miaka 30 Jela kwa kusafirisha Bangi

 

Mahakama ya Wilaya ya Rungwe imemhukumu Tecla Lumala (24), mkazi wa Morogoro, kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na hatia ya kusafirisha dawa za kulevya aina ya bangi.

Hukumu hiyo imetolewa Agosti 18, 2025 na Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Rungwe, Mhe. Mwinjuma Bwanga, baada ya kuridhishwa na ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka.

Kwa mujibu wa taarifa za mahakama, Tecla alikamatwa Desemba 22, 2024 akiwa anasafirisha kiasi cha kilogramu 6.8 za bangi kupitia kizuizi cha polisi cha Kayuki (Police Road Block) kilichopo katika Kijiji cha Ngujubwaje "A", Kata ya Ilima, Tarafa ya Pakati, Wilaya ya Rungwe.

Mshitakiwa alifikishwa mahakamani Januari 1, 2025 na kusomewa mashtaka mbele ya Hakimu Bwanga, ambapo alitiwa hatiani kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya kinyume cha sheria.

Akisoma hukumu hiyo, Mhe. Bwanga alisema kuwa Mahakama imezingatia uzito wa kosa na madhara ya dawa za kulevya kwa jamii, hivyo adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela ni ya haki na itatumika kama fundisho kwa wengine.

Wakati huo huo, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limeendelea kutoa wito kwa wananchi kutoa ushirikiano kwa kufika mahakamani kutoa ushahidi katika mashauri mbalimbali yanayowakabili watuhumiwa wa makosa ya jinai, ili kusaidia upatikanaji wa haki kwa mujibu wa sheria.

Aidha, jeshi hilo limewahimiza wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa kuhusu wahalifu ili waweze kukamatwa na kuchukuliwa hatua stahiki kisheria.

Chapisha Maoni

0 Maoni