Waziri Kikwete aitaka sekta ya Hifadhi ya Jamii kuwekeza miradi ya Maendeleo Endelevu

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Ridhiwani Kikwete, amezitaka nchi za Afrika kuwekeza michango ya wanachama wa mifuko ya hifadhi ya jamii katika miradi mikubwa ya maendeleo ili kuchochea ustawi wa bara hilo.

Akizungumza jana Julai 10, 2025, katika Mkutano wa 14 wa Kimataifa wa Watunga Sera wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii Barani Afrika unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), Mhe. Kikwete alisema mifuko hiyo ina uwezo mkubwa wa kuchangia maendeleo ya miundombinu kama barabara, reli, bandari na huduma za kijamii kama afya na elimu.

“Huu ni wakati wa kuhakikisha kuwa rasilimali hizi tunazozikusanya kutoka kwa wanachama wetu hazikai tu kwenye mabenki, bali zinafanya kazi na kuleta matokeo chanya katika maendeleo ya bara letu,” alisema Mhe. Kikwete.

Mkutano huo ulifunguliwa rasmi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango, huku ukiwakutanisha mawaziri, watunga sera na wataalamu wa sekta ya hifadhi ya jamii kutoka nchi mbalimbali za Afrika.

Kwa mujibu wa Waziri Ridhiwani, jukwaa hilo linatoa fursa kwa nchi wanachama kubadilishana uzoefu na kuja na mikakati ya pamoja itakayowezesha mifuko hiyo kufanya uwekezaji wenye tija.

Kauli mbiu ya mkutano huo ni: “Mifuko ya Hifadhi ya Jamii: Chachu ya Maendeleo ya Miundombinu na Ukuaji wa Kiuchumi na Kijamii Barani Afrika.




Chapisha Maoni

0 Maoni