Tanzania, UNESCO kuimarisha ushirikiano kwenye uhifadhi wa Urithi wa Dunia

 

Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Dk. Pindi Chana, leo Julai 10, 2025, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Msaidizi wa UNESCO anayeshughulikia masuala ya Utamaduni, Ernesto Ottone, pembezoni mwa Mkutano wa 47 wa Kamati ya Urithi wa Dunia unaoendelea jijini Paris, Ufaransa.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamekubaliana kuimarisha ushirikiano baina ya UNESCO na Tanzania, hususan katika uhifadhi wa Maeneo ya Urithi wa Dunia yaliyopo nchini, yakiwemo hifadhi na maeneo ya kihistoria yanayotambuliwa kimataifa.

Akizungumza baada ya kikao hicho, Waziri Chana alisema Tanzania ina hazina kubwa ya vivutio vya utalii na urithi wa kiutamaduni ambavyo vinahitaji kulindwa na kuendelezwa kwa ushirikiano wa kimataifa.

“Ushirikiano na UNESCO utasaidia si tu kuhifadhi maeneo haya, bali pia kuyaendeleza kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” alisema.

Kwa upande wake, Ottone alieleza dhamira ya UNESCO kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kukuza shughuli za kiutamaduni, pamoja na kuimarisha juhudi za kuhifadhi vivutio vyake vya kipekee vinavyovutia ulimwengu.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Ali J. Mwadini, pamoja na wataalam wa masuala ya urithi kutoka Tanzania.

Tanzania ni miongoni mwa nchi chache barani Afrika zilizo na idadi kubwa ya maeneo yaliyosajiliwa kama Urithi wa Dunia, yakiwemo Hifadhi ya Serengeti, Mlima Kilimanjaro na Mji Mkongwe wa Zanzibar.




Chapisha Maoni

0 Maoni