Serikali
imetoa rai kwa wananchi kote nchini kuchukua hatua madhubuti za kujikinga dhidi
ya magonjwa ya mlipuko, hasa ugonjwa wa Kipindupindu, kwa kuzingatia kanuni
bora za afya ikiwemo matumizi ya maji safi na salama pamoja na matumizi ya vyoo
bora.
Wito huo
umetolewa jana Julai 9, 2025 jijini Dar es Salaam na Dkt. Vida Mmbaga,
Mkurugenzi Msaidizi wa Sehemu ya Epidemiolojia na Udhibiti wa Magonjwa kutoka
Wizara ya Afya, alipokuwa akimwakilisha Mganga Mkuu wa Serikali katika kikao
kazi cha kitaifa cha Kuhakiki Maeneo Hatarishi ya Kupata Kipindupindu (PAMI’s).
Kikao
hicho kimeratibiwa kwa ushirikiano wa Wizara ya Afya na Shirika la Afya Duniani
(WHO), kwa lengo la kujadili na kuweka mikakati ya kudhibiti ugonjwa huo ambao
umekuwa ukiibuka mara kwa mara katika baadhi ya maeneo nchini.
Akizungumza
wakati wa kikao hicho, Dkt. Mmbaga alieleza kuwa ugonjwa wa Kipindupindu
unasababishwa na kinyesi kibichi cha binadamu kinachoingia kwenye maji, na
kusisitiza umuhimu wa wananchi kuchukua tahadhari kwa kutumia vidonge vya
kutibu maji, kudumisha usafi wa mazingira na kutumia vyoo bora.
“Sisi kama
Serikali, kupitia kikao hiki, tunakusudia kuweka mikakati ya pamoja ya kuzuia
Kipindupindu hasa katika maeneo ambayo yamekuwa yakikumbwa mara kwa mara na
mlipuko wa ugonjwa huu,” alisema Dkt. Mmbaga.
Aliongeza
kuwa Serikali imeendelea kutoa vidonge vya kutibu maji kwa wananchi kwa lengo
la kuimarisha kinga dhidi ya maambukizi, sambamba na kuunga mkono mkakati wa
kimataifa wa kutokomeza Kipindupindu ifikapo mwaka 2030.
“Mpango
wetu ni kuhakikisha tunatokomeza Kipindupindu kwa zaidi ya asilimia 90 ifikapo
2030. Hivyo, kikao hiki kina umuhimu mkubwa katika kubaini maeneo yaliyo
hatarini na kuweka mikakati madhubuti ya kudhibiti,” alisisitiza.
Kwa upande
wake, Mkuu wa Masuala ya Dharura kutoka Shirika la Afya Duniani Kanda ya Afrika
(WHO-AFRO), Dkt. Dick Chamla, ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendelea
kushirikiana na WHO katika kupambana na magonjwa ya mlipuko, ikiwemo
Kipindupindu.
“Serikali
ya Tanzania imeonyesha mfano wa kuigwa kwa kuwa mstari wa mbele katika
mapambano haya. Kupitia kikao hiki, tunaamini tutaweza kuainisha maeneo
hatarishi na kuchukua hatua sahihi kwa pamoja,” alisema Dkt. Chamla.
Kwa mujibu
wa WHO, Kipindupindu bado ni tishio kwa maisha ya watu wengi barani Afrika,
hivyo ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na wadau wa afya unahitajika ili
kudhibiti mlipuko huo kwa ufanisi.
0 Maoni