Serikali kutoa mafunzo kwa mabloga kuelekea Uchaguzi Mkuu 2025

 

Serikali imesema itatoa mafunzo maalumu kwa waandishi wa blogu nchini ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika usambazaji wa habari sahihi kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, katika Mkutano wa Wadau wa Habari uliofanyika jana Julai 9, 2025 katika ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.

Mkutano huo uliangazia nafasi ya sekta ya habari katika kufanikisha uchaguzi huru na wa haki, huku hoja ya kuwajengea uwezo mabloga ikitawala mjadala.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mwenyekiti wa Chama cha Mabloga Tanzania (TBN), Beda Msimbe, alisema licha ya kuwa baadhi ya mabloga si waandishi wa habari kitaaluma, wamekuwa wakihusika moja kwa moja katika usambazaji wa taarifa kupitia majukwaa ya kidijitali.

"Katika dunia ya sasa ya teknolojia na akili bandia (AI), watu wengi wanategemea taarifa kutoka kwenye blogu na tovuti zaidi ya mitandao ya kijamii. Ni muhimu mabloga hawa wakapatiwa mafunzo ili kuongeza weledi hasa katika uandishi wa masuala ya siasa kuelekea uchaguzi mkuu," alisema Msimbe.

Aliongeza kuwa mabloga wanabeba dhamana kubwa kutokana na idadi yao na nafasi waliyonayo katika kuunda mitazamo ya wananchi kuhusu masuala ya kijamii na kisiasa.

Katika majumuisho yake, Katibu Mkuu Msigwa aliiagiza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuandaa mafunzo hayo mapema iwezekanavyo ili kuwaandaa mabloga kwa jukumu hilo muhimu.

Wadau mbalimbali waliohudhuria mkutano huo wameeleza kuwa hatua hiyo ya Serikali ni ishara ya kutambua rasmi mchango wa mabloga katika mchakato wa kidemokrasia na maendeleo ya tasnia ya habari nchini.

Kwa mujibu wa TBN, chama hicho kina wanachama zaidi ya 200 walioko ndani na nje ya nchi, hivyo mafunzo hayo yanatarajiwa kuwa na athari chanya kwa upatikanaji wa taarifa sahihi na zenye kuzingatia maadili ya uandishi wa habari kipindi cha uchaguzi na baada ya hapo.

Mkutano huo ulifunguliwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk Doto Biteko, ambaye alisisitiza umuhimu wa vyombo vya habari na vyombo vya usalama kushirikiana katika kulinda amani na kuhimiza uvumilivu kuelekea uchaguzi huo.

Chapisha Maoni

0 Maoni