Tanzania yawa ya kwanza Afrika kuandaa Mkutano wa Kwanza wa Dunia wa Diakonia

 

Kwa mara ya kwanza katika historia, Mkutano Mkuu wa Dunia wa Diakonia (Diakonia World Assembly) umefanyika ardhi ya Afrika, ambapo mji wa Moshi, Tanzania umetumika kuwa mwenyeji wa tukio hilo la kihistoria. 

Mkutano huo wa siku tano unaoendeshwa kwa kaulimbiu isemayo “Kucheza kwa Imani, Kupiga Ngoma ya Tumaini” umejumuisha wajumbe 250 wakiwemo mashemasi wa kiume na mashemasi wa kike kutoka mataifa mbalimbali duniani. 

Hafla rasmi ya ufunguzi wa mkutano huo ilifanyika Julai 7–12, 2025 katika Kanisa Kuu la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) jijini Moshi, ambapo aliyekuwa Askofu Mkuu wa KKKT, Dkt. Frederick Shoo, aliwakaribisha washiriki na kusisitiza umuhimu wa tukio hilo. 

“Mkutano huu wa Diakonia ni fursa kwa mashemasi kujifunza kwa pamoja na kubadilishana mbinu mbalimbali za huduma za kichungaji kutoka maeneo mbalimbali ya dunia,” alisema Askofu Dkt. Shoo. “Ni heshima kubwa kwa KKKT kuwa mwenyeji wa tukio hili la kihistoria. Tunaamini kwamba uwepo wa mkutano huu katika ardhi yetu ni baraka kwa Kanisa na jamii nzima.”

 Naye Katibu Mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni (WCC), Mchungaji Profesa Dkt. Jerry Pillay, aliipongeza KKKT kwa kujitoa kikamilifu katika huduma za diakonia zinazobadilisha maisha ya watu kwa njia chanya. 

“Kanisa (KKKT) linafanya kazi ya kipekee yenye kugusa maisha na kubadilisha jamii kwa undani,” alisema Mchungaji Prof. Pillay. 

Aliwahimiza mashemasi kuendelea kudumisha imani, kueneza matumaini yasiyozimika na kuishi kwa upendo, akitoa wito kwa Wakristo duniani kote kukabiliana na changamoto za dunia ya sasa kwa imani na kuwa mawakala wa tumaini na huruma. 

Mkutano huu wa Diakonia unaoratibiwa na Shirikisho la Diakonia Duniani (World Diakonia Federation) umehusisha washiriki kutoka madhehebu na nchi mbalimbali, huku ukiambatana na vipindi vya ibada, mada kuu, warsha, shughuli za kiutamaduni na majadiliano kuhusu namna ya kuimarisha huduma ya diakonia katika dunia inayobadilika kwa kasi. 

Tukio hili limewekwa kwenye historia kama hatua muhimu katika harakati za kimataifa za huduma ya imani na linathibitisha nafasi inayokua ya Afrika katika kuunda mustakabali wa huduma za kidini na mabadiliko ya jamii.



Chapisha Maoni

0 Maoni