Serikali yaanza rasmi ujenzi wa daraja Jangwani

Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imeanza rasmi ujenzi wa daraja jipya la kisasa katika eneo la Jangwani jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kutatua tatizo sugu la mafuriko linalolikumba jiji hilo hasa nyakati za mvua kubwa.

Daraja hilo, litakalokuwa na urefu wa mita 390, linajengwa kwa viwango vya juu vya kisasa likilenga kuhakikisha uimara, usalama na matumizi ya muda mrefu, hasa kwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabianchi zinazoendelea kuathiri maeneo mengi ya mijini.

Meneja wa TANROADS Mkoa wa Dar es Salaam, Mhandisi Alinanuswe Kyamba, ameeleza kuwa tayari mkandarasi wa mradi amepokea malipo ya awali na kazi ya awali ya kutengeneza barabara ya muda (diversion) kwa ajili ya magari imeanza.

“Daraja hili ni la kimkakati kwa kuwa linashughulikia tatizo la muda mrefu la mafuriko eneo la Jangwani. Pia litasaidia kuboresha usafiri kwa wakazi wa Dar es Salaam, kwa kuwa litajumuisha pia njia za magari, maingilio pamoja na njia salama za waenda kwa miguu,” alisema Mhandisi Kyamba.

Ameeleza kuwa mradi huo ni sehemu ya jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuboresha miundombinu ya jiji la Dar es Salaam na kulifanya kuwa na uwezo wa kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

Jangwani ni miongoni mwa maeneo yanayokumbwa mara kwa mara na mafuriko wakati wa mvua, hali inayosababisha usumbufu kwa wakazi, hasara kwa wafanyabiashara pamoja na kuathiri shughuli za usafirishaji. Ujenzi wa daraja hili unatarajiwa kuwa suluhisho la kudumu kwa tatizo hilo.

Chapisha Maoni

0 Maoni