Polisi wawili
wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma kwa tuhuma za kuhusika katika
tukio la kumpiga risasi na kusababisha kifo cha Frank Sanga (32), mkazi wa
Kitongoji cha Mgomwa, Kata ya Matumbulu, jijini Dodoma.
Tukio hilo la kusikitisha
linadaiwa kutokea Julai 19, 2025, majira ya saa 7:30 mchana katika maeneo ya
Matumbulu, wakati marehemu Frank alipojaribu kumsaidia ndugu yake aliyekuwa
amekamatwa na askari hao kwa makosa ya usalama barabarani, kwa lengo la kuzuia
asipelekwe kituoni.
Kwa mujibu wa maelezo
yaliyotolewa leo Julai 21, 2025, na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gallus
Hyera, askari hao walimkamata mwendesha pikipiki (jina linahifadhiwa kwa sababu
za kiuchunguzi) kwa makosa ya kutokuwa na leseni, kutokuvaa kofia ngumu, na
kuendesha chombo kibovu.
Kamanda Hyera amesema
baada ya kukamatwa, dereva huyo alipiga simu kwa ndugu zake ambao walifika kwa
wingi wakiwa kwenye pikipiki tano, kila moja ikiwa na watu zaidi ya wawili, na
kujaribu kwa nguvu kuichukua pikipiki hiyo na kumwachia huru ndugu yao.
“Katika hali hiyo ya
vurugu na kuonekana kama walikuwa wamejipanga kupambana na askari, askari
walilazimika kujihami kwa kufyatua risasi, ambapo Frank Sanga alijeruhiwa
kwenye paja na ugoko wa mguu wa kushoto. Alikimbizwa hospitalini kwa matibabu
lakini alifariki dunia wakati akiendelea kupatiwa huduma,” amesema Kamanda
Hyera.
Ameongeza kuwa Jeshi la
Polisi limechukua hatua za awali kwa kuwasimamisha kazi askari hao na
kuwashikilia kwa uchunguzi zaidi, huku likiahidi kuchukua hatua stahiki endapo
watabainika kuwa walikiuka maadili ya kazi zao.
Tukio hili limezua
taharuki kwa wakazi wa Matumbulu, huku baadhi wakitaka uchunguzi huru kufanyika
na haki kutendeka kwa familia ya marehemu.
0 Maoni