Mwenyekiti wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM) Taifa ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametangaza kuwa CCM imeamua kufanya marekebisho ya
Katiba yake ili kuruhusu Kamati Kuu ya chama hicho kuteua wagombea wengine
zaidi ya majina matatu yaliyopitishwa na Kamati za Siasa za Wilaya na Mkoa,
pale ambapo kutakuwa na ulazima wa kufanya hivyo.
Akizungumza leo katika
Mkutano Mkuu wa CCM uliofanyika jijini Dodoma, Dkt. Samia alisema mabadiliko
hayo yanakusudia kuongeza ufanisi na kutoa nafasi kwa Kamati Kuu kuwa na
mamlaka mapana zaidi ya uteuzi, hasa ikizingatiwa idadi kubwa ya wanachama
wanaojitokeza kugombea nafasi mbalimbali.
“Tulitanua demokrasia,
wajumbe wa kuchagua wawe wengi zaidi. Jambo lile limevutia wanachama wengi wa
CCM kuomba kugombea, na kuna maeneo yenye wagombea hadi 40. Tumeona kwenda na
watatu kati ya wengi hao si busara, halafu papohapo Kamati Kuu imebanwa na
Katiba, hatuwezi kuongeza majina,” alisema Rais Dkt. Samia.
Aliendelea kufafanua kuwa
uamuzi huo ni sehemu ya mageuzi ndani ya chama yanayolenga kuendana na hali
halisi ya kisiasa nchini. “Tumerudi kwenu kuomba ridhaa ya hilo, na sasa
tunataka jambo hili lijadiliwe. Mjadala upo wazi,” aliongeza.
Kwa sasa, wajumbe wa
Mkutano Mkuu wa CCM wanaendelea na zoezi la kupiga kura ya ama kuidhinisha au
kukataa pendekezo hilo la marekebisho ya Katiba.
Mabadiliko haya, iwapo yatapitishwa,
yanatarajiwa kuongeza ushawishi wa Kamati Kuu katika mchakato wa uteuzi wa
wagombea wa CCM kuelekea uchaguzi mkuu ujao.
0 Maoni