Wakala wa Huduma za
Misitu Tanzania (TFS) umetumia jukwaa la Maonesho ya Ujuzi, Fani na Ajira kwa
Vijana yanayoendelea katika viwanja vya Mwembe Togwa, Manispaa ya Iringa,
kutangaza fursa mbalimbali za kiuchumi zinazopatikana kupitia uhifadhi wa
misitu nchini.
Maonesho hayo yaliyoanza
Julai 25 hadi 27, 2025, yanalenga kuhamasisha vijana wa Mkoa wa Iringa na
maeneo jirani kujikita katika sekta zinazoweza kuwainua kiuchumi, zikiwemo
ufugaji nyuki, biashara ya mazao ya misitu, upandaji miti, pamoja na utalii wa
ikolojia.
Akizungumza wakati wa
ufunguzi wa maonesho hayo, Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Mhe. Estomih Kyando, aliyemwakilisha
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, aliipongeza TFS kwa kuendelea kutoa elimu na kufungua
milango ya fursa kwa vijana kupitia ushiriki wao katika maonesho hayo.
“Mkoa wetu wa Iringa una
historia nzuri ya uhifadhi wa misitu na wananchi wake wameonyesha mwitikio
mkubwa katika biashara ya mazao ya misitu ya kupandwa. TFS imekuwa mstari wa
mbele kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi za fursa hizi,” alisema Mhe.
Kyando.
Alisisitiza kuwa vijana
wanapaswa kuwa mabalozi wa elimu ya uhifadhi na wawe mstari wa mbele
kuchangamkia fursa zinazopatikana katika sekta mbalimbali zinazochochewa na
dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan
ya maendeleo jumuishi kwa vijana kupitia ujuzi, ajira na uchumi wa viwanda.
Kwa upande wake, Mhifadhi
Paulo Rugola kutoka TFS, akizungumza wakati wa ziara ya viongozi wa serikali
katika banda lao Julai 26, 2025, alieleza kuwa TFS inatumia majukwaa ya
maonesho kama haya kuwafikia wananchi na kuwahamasisha kuhusu matumizi endelevu
ya misitu kwa ajili ya maendeleo yao ya kiuchumi.
“Tunatangaza fursa
mbalimbali zilizopo katika misitu yetu. Hizi ni pamoja na upatikanaji wa
malighafi kutokana na miti, ufugaji nyuki na uuzaji wa mazao yake, pamoja na
utalii wa ikolojia ambao unaendelea kukua kwa kasi nchini,” alisema Rugola.
Aliongeza kuwa TFS ina
vituo maalum vya uzalishaji wa mbegu bora za miti kwa ajili ya wananchi
wanaotaka kuwekeza kwenye kilimo cha miti, hasa katika maeneo ya Nyanda za Juu
Kusini ambapo uelewa kuhusu faida ya misitu umeongezeka.
“Tunawakaribisha vijana
na wakulima wote kuja kujifunza kuhusu uzalishaji bora wa miti, kwani upandaji
miti siyo tu unaongeza kipato, bali pia ni sehemu ya juhudi za kukabiliana na
mabadiliko ya tabianchi,” alisisitiza Rugola.
Aidha, alikemea matumizi
holela ya moto katika maeneo ya misitu hasa msimu huu wa kiangazi, akihimiza
wananchi kuchukua tahadhari na kufuata elimu ya uhifadhi wanayopewa na maafisa
wa TFS.
“Kumekuwa na matukio
mengi ya moto ambayo yanaharibu juhudi kubwa za kuhifadhi misitu. TFS
inaendelea kutoa elimu ya matumizi sahihi ya moto ili kulinda rasilimali hizi
kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo,” aliongeza.
TFS ni miongoni mwa
taasisi nyingi za serikali na binafsi zinazoshiriki katika maonesho hayo
yaliyoandaliwa kwa kauli mbiu: “Kijana: Ujuzi Wako, Fani Yako, Chaguo Lako.”
Maonesho haya yanatarajiwa kufungwa rasmi Julai 27, 2025.
0 Maoni