DCEA yakamata tani 37 za dawa za kulevya, raia wa kigeni watajwa

  

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama, imefanikiwa kukamata jumla ya kilo 37,197.142 za dawa za kulevya katika operesheni zilizofanyika maeneo mbalimbali nchini kati ya Mei hadi Julai 2025. 

Katika taarifa iliyotolewa leo na Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali cha Mamlaka hiyo, dawa hizo ni pamoja na kilo 11,031.42 za Mitragyna Speciosa (aina ya dawa mpya za kulevya), bangi kilo 24,873.56, mirungi kilo 1,274.47, skanka kilo 13.42, heroin kilo 2.21 na methamphetamine gramu 1.42. 

Aidha, dawa za tiba zenye asili ya kulevya zilizokamatwa ni pamoja na ketamine kilo 1.92 na vidonge 1,000 vya flunitrazepam (maarufu kama rohypnol). Pia, zilikamatwa lita 6 za kemikali bashirifu aina ya hydrochloric acid. 

Katika operesheni hiyo, ekari 1,045.5 za mashamba ya bangi ziliteketezwa katika mikoa mbalimbali ikiwemo Ruvuma, Mbeya, Mara, Kagera, Dodoma, Tabora, Morogoro na Arusha. 

Shehena Kutoka Sri Lanka Yakamatwa Temeke 

Katika operesheni maalum iliyofanyika kwenye bandari kavu ya Temeke, Dar es Salaam, zilikamatwa kilo 11,031.42 za Mitragyna Speciosa zilizokuwa zimeingizwa nchini kutoka Sri Lanka, zikiwa zimefungwa kwenye maboksi yenye nembo ya mbolea. Mmea huu, unaojulikana pia kama Kratom, una kemikali zinazojulikana kwa majina ya Mitragynine na 7-Hydroxymitragynine, ambazo huathiri mfumo wa fahamu, husababisha uraibu na hata vifo vya ghafla. 

Watuhumiwa 64 Wakamatwa 

Katika operesheni hiyo ya kitaifa, jumla ya watuhumiwa 64 walikamatwa wakihusishwa moja kwa moja na usambazaji au umiliki wa dawa hizo. 

Katika tukio jingine jijini Dar es Salaam, eneo la Posta, watuhumiwa sita waliokamatwa walijumuisha raia wawili wa China waliotajwa kwa majina ya Chein Bai na Qixian Xin. Walikutwa na methamphetamine gramu 1.42, vidonge 1,000 vya rohypnol, na ketamine kilo 1.92. 

Kiwanda Bubu cha Biskuti za Bangi 

Katika eneo la Sinza, jijini Dar es Salaam, watu wawili walikamatwa wakiwa wamiliki wa kiwanda bubu kilichokuwa kikitengeneza biskuti zilizochanganywa na bangi na kuzisambaza katika mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza, Lindi na Mtwara. Mkoani Lindi, mfanyabiashara wa madini naye alikamatwa akisambaza biskuti zenye bangi. 

Heroin Kutoka Msumbiji Yazuiwa 

Katika hatua nyingine, kilo 26 za heroin zilizokuwa zikisafirishwa kutoka Msumbiji kuelekea Tanzania zilizuiawa kabla ya kuingia nchini. 

Maiti Zaanza Kutumiwa Kusafirisha Dawa 

DCEA pia imebaini kuwa baadhi ya magenge ya kihalifu yamerudi kutumia mbinu hatarishi za kusafirisha dawa za kulevya kwa kutumia maiti za binadamu, maarufu kama "begi". 

Aidha, mamlaka hiyo imeonya kuwa raia wa kigeni wamekuwa wakiwatumia Watanzania kusafirisha au kusambaza dawa za kulevya kwa njia ya mahusiano ya kirafiki, kisha kuwatumia katika kampuni, usafiri wa bodaboda, bajaji, teksi na hata kupitia wasambazaji wa vifurushi. 

Mamlaka Yaonya Umma 

DCEA imewataka wananchi kuwa waangalifu na mizigo wanayotumwa au wanayopokea, hasa kutoka kwa watu wasiowafahamu vyema, ili kuepuka kuingizwa katika biashara hiyo haramu. 

Mamlaka hiyo imewataka Watanzania kuendelea kushirikiana na vyombo vya dola kwa kutoa taarifa za wale wote wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya, huku ikiahidi kuchukua hatua kali za kisheria kwa yeyote atakayebainika kuhusika.

Chapisha Maoni

0 Maoni