Serikali yapendekeza mgao mpya wa mapato ya NCAA

Serikali imependekeza kufanya marekebisho ya Kifungu cha 12 cha Sheria ya Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA), Sura 284, kwa lengo la kubadilisha mgawanyo wa mapato yatokanayo na huduma zinazotolewa na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA). 

Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, ametoa pendekezo hilo Bungeni leo alipowasilisha Mapendekezo ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka 2025, mbele ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linaloendelea jijini Dodoma. 

Kupitia marekebisho hayo, Serikali inapendekeza kufuta kifungu kidogo cha (b) kilichokuwa kinaitaka mgao wa asilimia 91 ya mapato kuwekwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. 

Badala yake, sasa mapato yatokanayo na huduma zinazotolewa TANAPA asilimia 51 itawekwa katika akaunti iliyopo Benki Kuu ya Tanzania (BoT), na matumizi yake yatahitaji kibali kutoka kwa Mlipaji Mkuu wa Serikali. 

Aidha, asilimia 40 ya mapato hayo itaendelea kupelekwa moja kwa moja katika Mfuko Mkuu wa Serikali.

 “Lengo la hatua hii ni kuiwezesha NCAA kuwa na uwezo wa kifedha wa kutekeleza majukumu yake ya msingi katika uhifadhi, maendeleo ya jamii na utalii endelevu,” alisema Dkt. Nchemba. 

Mabadiliko haya yanakuja wakati kukiwa na mjadala mpana kuhusu mustakabali wa eneo la Ngorongoro, ambalo ni urithi wa dunia unaokabiliwa na changamoto za kiikolojia na kijamii kutokana na shughuli za binadamu na ongezeko la watu. 

Wadau wa uhifadhi, haki za jamii na maendeleo wameelezea matumaini kuwa mfumo huu mpya wa mgao wa mapato utasaidia kuboresha utendaji wa NCAA bila kuathiri mchango wake kwa Serikali Kuu.

 


Chapisha Maoni

0 Maoni