Semfuko awatunuku vyeti vya pongezi wanamichezo wa TAWA

 

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Meja. Jenerali (Mstaafu) Hamis Semfuko leo Juni 24,2025, jijini Dar es Salaam amewatunuku vyeti vya pongezi wanamichezo (14) waliofanya vizuri kwenye michezo ya riadha (2) na mchezo wa kuvuta kamba (12) katika Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Mashirika ya Umma, Taasisi na Makampuni Binafsi Tanzania (SHIMMUTA) yaliyofanyika mnamo mwezi Novemba 2024.

Akizungumza wakati wa utoaji wa vyeti hivyo, Mej.Jen (Mstaafu) Semfuko  amesema michezo ni miongoni mwa nyenzo kubwa katika kuongeza mshikamano kwenye Majeshi.

" Kazi kubwa ya michezo katika majeshi ni kuunganisha jeshi kwa pamoja, kwa lugha ya kigeni tunasema esprit de corps," amesema  Semfuko.

Kadhalika, Mej. Jen (Mstaafu) Semfuko amewapongeza wanamichezo hao kwa kushinda Medali na Kombe na akasisitiza kuwa Bodi ya Wakurugenzi itahakikisha wanamichezo  wanaendelea kupata motisha mbalimbali ili kuongeza morali ya ushindi katika mashindano  ambayo TAWA ni mshiriki.

" Menejimenti itafanya bidii, ili kuhakikisha tunashinda michezo mingine na kwa kuanza, Bodi inatoa zawadi hii ndogo kwenu nyote kwa kutuletea ushindi huu," amesema Semfuko.

Sambamba na hilo, Semfuko amewataka wanamichezo hao kuwa mfano kwa watumishi wengine kwa kuwahamasisha ili washiriki katika michezo mbalimbali.

Awali, akimkaribisha Mej. Jen (Mstaafu) Semfuko, Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA, Mlage Kabange amesema TAWA inashiriki kwenye mashindano ya michezo mbalimbali kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii vinavyosimamiwa na TAWA, kuimarisha afya za Askari na kuimarisha mahusiano kati ya TAWA na Taasisi zingine.

Aidha, Kamishna Kabange ameongeza kuwa katika Mashindano ya mwaka huu Menejimenti imejipanga vizuri  ili kuhakikisha vikosi vya TAWA vinakuwa bora na kujiweka katika nafasi ya ushindi zaidi.

Naye , Mratibu wa michezo - TAWA, Carlos Mbiro ameishukuru Bodi ya Wakurugenzi kwa kuwatunuku zawadi hizo na akasema kama wanamichezo wanafarijika sana na wanaahidi kuendelea kufanya vizuri katika mashindano mengine yatakayofanyika.

                        Na. Joyce Ndunguru - Dar es Salaam

Chapisha Maoni

0 Maoni