Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameipongeza Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa juhudi zake za kuwafuata wananchi popote walipo
na kuwapatia huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo bila malipo.
Rais Dkt. Samia alitoa
pongezi hizo jana katika hafla ya kupokea gawio na michango kutoka kwa Taasisi,
Mashirika ya Umma na Kampuni ambazo Serikali inamiliki hisa, iliyofanyika Ikulu
jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika
hafla hiyo, Mhe. Rais alisema taasisi zinazotoa huduma zenye manufaa kwa jamii
zinastahili kutambuliwa na kupongezwa, kama ambavyo JKCI imekuwa ikifanya
kupitia huduma zake za tiba mkoba.
"Taasisi ambazo
zinatoa mchango wao kwa jamii kutokana na huduma wanazotoa nazo zinatakiwa
kuonekana na kuonesha wanachangia kiasi gani kwa umma. JKCI wamekuwa mstari wa
mbele na huduma yao inagusa wananchi moja kwa moja," alisema Rais Dkt. Samia.
Kwa upande wake,
Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alisema JKCI imefanikiwa kutoa gawio
la Shilingi Bilioni 2 kupitia huduma za moyo zilizotolewa kwa wananchi 27,600
katika mikoa 16 nchini kupitia kambi maalum ya Tiba Mkoba ya Mhe. Rais Samia.
"JKCI hata
tusipowaona kwenye makusanyo ya fedha, tunaona matokeo yao kwenye maisha ya
watu. Huduma ya tiba mkoba imefika mikoa 16 na kuwanufaisha maelfu ya
Watanzania," alisema Mchechu.
Aidha, Mchechu
alibainisha kuwa kwa mara ya kwanza JKCI imeweza kupanua wigo wa huduma zake
kwa kuanzisha kliniki nje ya makao makuu, hatua inayodhihirisha ukuaji na
mafanikio ya taasisi hiyo.
“Sasa hivi ukihitaji
huduma za JKCI, unaweza kuzifuata katika matawi yao yaliyopo Oysterbay, Kawe,
Dar Group Hospitali, na Arusha AICC,” aliongeza.
Msajili huyo
alisisitiza kuwa ofisi yake itaendelea kufuatilia namna mafanikio ya taasisi
kama JKCI yanavyoweza kuwagusa moja kwa moja watendaji wake ili kuongeza
ufanisi na kuchochea uwajibikaji zaidi katika utumishi wa umma.
0 Maoni