Kamishna Kuji awapiga msasa Maafisa na Askari Uhifadhi TANAPA kuelekea msimu mpya wa utalii

 

Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Musa Nassoro Kuji jamefanya kikao kikazi na Maafisa na Askari wa Hifadhi ya Taifa Kitulo iliyopo mkoani, Njombe.

Katika kikao kazi hicho kilichofanyika jana Kamishna Kuji amewataka Maafisa na Askari kujipanga vilivyo katika kufanya kazi hasa katika msimu huu mpya wa utalii ambao unakwenda kuanza mwezi Julai 2025 ili kuhakikisha mapato ya Serikali yanakusanywa kikamilifu.

“Ni fahari kubwa kwetu TANAPA kushiriki kuchangia katika ujenzi wa Taifa letu kupitia uratibu na usimamizi wa shughuli za utalii katika hifadhi za Taifa na maeneo ya Malikale yaliyokasimiwa kwa TANAPA. Mafanikio hayo ni matunda ya kila mmoja wetu katika kuhifadhi maliasili hizi tulizokabidhiwa kuzitunza kwa niaba ya Watanzania. Mpaka siku ya jana (juzi) 23.06.2025 Shirika limeweza kukusanya shilingi billioni 480 ikiwa imesalia shilingi 20 kufikisha nusu trillioni” alisema Kamishna Kuji.

“Bodi ya Wadhamini ya Shirika imenituma niwahakikishie ushirikiano wa kutosha “full support” katika kufanikisha utendaji kazi wa viwango vya Kimataifa. Tunapoanza mwezi wa saba TANAPA tunategemea kususanya trilioni ili tuondoke kwenye ukusanyaji wa mabilioni, hiyo ndiyo kazi iliyo mbele yetu. Hili linawezekana kwa kila mmoja wetu kuchapa kazi usiku na mchana ili kufikia malengo ya Shirika na Taifa kwa ujumla,” aliongeza Kamishna Kuji.

Awali, akimkaribisha Kamishna wa Uhifadhi katika Hifadhi ya Taifa Kitulo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi na Mkuu wa Kanda ya Kusini, Godwell Meng’ataki alipongeza jitihada zinazofanywa na Serikali katika kuboresha Uhifadhi na Utalii hususani kwa hifadhi zilizopo kusini kwani hifadhi hizo zimekuwa zikipokea idadi kubwa ya watalii.

“Baada ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano Dkt. Samia Suluhu Hassan kucheza Filamu maarufu ya Tanzania: The Royal Tour” na ile ya “Amazing Tanzania” Hifadhi za Taifa zilizopo Kusini tumeanza kuona matunda yake kwa kuongeza idadi ya watalii lakini pia kwa namna ambavyo Bodi ya Wadhamini ya TANAPA imekuwa ikitoa miongozo kwa Menejimenti ya Shirika ili kutoa huduma zenye viwango vya Kimataifa kwa watalii. Jitihada hizo zimekuwa chachu ya kuvutia watalii wengi katika maeneo yetu” alisema Kamishna Meng’ataki.

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Kitulo Afisa Uhifadhi Daraja la Kwanza, Ally Hemedi Kimwanga alieleza kuwa “Katika mwaka fedha ujao wa 2025/2026, unaotarajiwa kuanza mwezi wa Julai 2025 Hifadhi ya Taifa Kitulo imejipanga vilivyo katika kuhifadhi na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea hifadhi hiyo pamoja na mapato yatokanayo na shughuli za utalii. Maafisa na Askari Uhifadhi wa Hifadhi ya Taifa Kitulo tunakuahidi Afande Kamishna kuchapa kazi yenye viwango vya Kimataifa”.

Pia, Kamishna wa Uhifadhi Musa Nassoro Kuji leo amefanya ziara ya kikazi na kufanya kikao na Maafisa na Askari Uhifadhi wa Kanda ya Kusini ya TANAPA iliyopo Rujewa wilayani Mbarali, Mkoani Mbeya.

Hifadhi ya Taifa Kitulo ni hifadhi yenye kivutio kikubwa cha uwepo wa maua mazuri yanayovutia na kupelekea hifadhi hiyo kupewa jina maarufu kama “Bustani ya Mungu”. Pia, hifadhi hiyo ni miongoni mwa vyanzo vya maji ya Ziwa Nyasa na Mto Ruaha Mkuu ambapo maji hayo ni muhimu sana kwenye kuchechemua shughuli za uchumi wa nchi ikiwemo uzalishaji wa umeme, shughuli za kilimo pamoja na uvuvi.


                  Na. Edmund Salaho/Kitulo

Chapisha Maoni

0 Maoni