Ulipaji fidia wanaopisha upanuzi Hifadhi ya Taifa Milima ya Mahale waanza

 

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma (RC), Thobias Andengenye jana Februari 25, 2025 amezindua ulipaji fidia kwa wakazi wa vitongoji vya Mahasa na Kabuyungu katika kijiji cha Kalilani, kata ya Buhingu wilayani Uvinza, Kigoma.

Wananchi wa kata ya Buhingu wanatakiwa kuhama kupisha eneo lenye ukubwa wa ekari 20 kwa ajili ya ikolojia ya wanyamapori adimu aina ya Sokwe walio hatarini kutoweka, ili waweze kuongezeka vizuri ndani ya Hifadhi ya Taifa Milima ya Mahale.

Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa ikiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Thobias Andengenye ilifika katika kijiji cha Kalilani na kuishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali wananchi wake, ambapo shilingi bilioni 1.68 zitatolewa kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi hao.

"Serikali ina mipango mizuri kwa wananchi wake, haiwezi kuwatoa hapa bila ya fedha mkapate shida muendako, fedha hizi zimekuja ili kuwapa nguvu ya kuanza kule mlipopangiwa," alisema RC Andengenye.

Alifafanua kuwa serikali imekuwa ikilipa fidia katika maeneo mengi nchini kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa, hivyo kijiji cha Kalilani na vitongoji vyake viwili sio eneo la kwanza kulipwa fidia.

"Leo tumekuja kuonesha kuwa serikali inayo dhamira ya dhati, kwa wale ambao tayari wamefanyiwa tathmini, Serikali inayojali maisha ya wananchi na kusimamia haki zote, ndio maana zoezi hili ni la wazi sio la kificho, wataalamu wapo kujibu maswali yenu na kuwasaidia," Andengenye aliwaambia wananchi hao.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Uvinza Mhe. Dihah Mathalani alibainisha kuwa sio wananchi wote wameridhia na kufanyiwa tathmini kwani wapo waliokataa kwa sababu zao, hivyo alitoa rai kwa waliofanyiwa tathmini kutokusikiliza uchochezi, kuvunjwa moyo na kupuuza uvumi unaosambaa kutoka kwa baadhi ya wananchi wasiotaka uhamishwaji huo kufanikiwa.

"Serikali ina taratibu zake, na taratibu zote zimefuatwa, hivyo tukae pamoja tusikilizane, tushirikiane ili zoezi liende vizuri, hakuna jambo litaharibika tukiwa wamoja," alisisitiza.

Akifafanua zaidi, Afisa Mhifadhi Mkuu, Halid Jumanne Mngofi ambaye ni Kaimu Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Milima ya Mahale, alisema kati ya kaya 375 zilizotakiwa kufanyiwa tathmini, ni 205 zimeridhia kufanyiwa tathmini na ziko tayari kulipwa fidia ziweze kuhama.

Eneo watakaloliacha ni muhimu kwa ustawi wa Sokwe wanaopatikana Hifadhi ya Milima ya Mahale.

"Vitongoji hivi viwili vya Hamasa na Kabuyungu vipo katika mwambao wa Milima ya Mahale na mwambao wa Ziwa Tanganyika, ambapo mwingiliano wa wananchi umekuwa mkubwa na wananchi wanazidi kuongezeka, hii italeta athari katika uhifadhi, ni vyema serikali imeliona mapema na kulifanyia kazi," alisema Halid.

Kuimarika kwa mazingira asilia ya Hifadhi ya Taifa Milima ya Mahale kutawafanya Sokwe kuongezeka, na watalii wengi kumiminika, hivyo kuongeza pato la Taifa.





        Na. Brigitha Kimario - Kigoma

Chapisha Maoni

0 Maoni