Waliomuua mfanyabiashara ya madini Chunya wakamatwa

 

Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya linawashikilia watuhumiwa watatu kwa tuhuma za mauaji ya mfanyabiashara ya madini Peter Bruno Mteta (59) mkazi wa Matundasi Wilayani Chunya.

Kamanda wa Polisi Mbeya SACP Benjamin Kuzaga ameeleza kuwa tukio hilo lilitokea Oktoba 12, 2024 saa 2:00 usiku kwa kumpiga risasi mgongoni mfanyabiashara huyo akiwa nyumbani kwake.

Amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Kenedy Richard maarufu Majiulaya (26) mkazi wa Kijiji cha Galula Wilaya ya Songwe mkoani Songwe, Msafiri Peter Mwahonje maarufu Wakwetu (48) mkazi wa Matundasi na Uhuru Ulaya Sukwa (63) mkazi wa Magamba Wilaya ya Mbozi Mkoa wa Songwe.

SACP Kuzaga amesema baada ya tukio hilo, Jeshi la Polisi lilianza upelelezi wa na Novemba 01, 2024 Kijiji cha Ubaruku Wilaya ya Mbaralimkoani Mbeya watuhumiwa watatu walikamatwa kuhusiana na tukio hilo wakiwa na silaha iliyotumika katika tukio hilo pamoja na risasi zake tano.

Sambamba na hilo, Jeshi la Polisi linamshikilia Hamis Shizya Kasunga (50) mkazi wa Maghorofani Jijini Mbeya kwa tuhuma za kumuua mke wake aitwaye Emmy Fred Mwasile (35) mkazi wa Forest Maghorofani Jijini Mbeya kwa kumpiga kwa kitu kizito sehemu mbalimbali za mwili wake.

Kamanda Kuzaga ameeleza kuwa tukio lililotokea Novemba 20, 2024 saa 6:30 mchana huko Mtaa wa Foresy mpya, Jijini Mbeya kutokana na wivu wa mapenzi akimtuhumu mke wake kuwa na mahusiano na mwanaume mwingine.

Amesema baada ya tukio hilo, mtuhumiwa alikimbia na katika ufuatiliaji alikamatwa Novemba 23, 2024 saa 9:00 alasiri katika mji mdogo wa Tunduma Mkoani Songwe akiwa katika harakati za kuvuka mpaka kwenda nchini Zambia.

Chapisha Maoni

0 Maoni