Wizara yajikita kutoa elimu ya malezi kwa vijana balehe

 

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum inaendelea na mkakati wake wa kuwajengea uwezo wa kutoa elimu mahsusi ya malezi kwa vijana balehe Maafisa Maendeleo ya Jamii, Maafisa Ustawi wa Jamii na waratibu wa Afya ya Mama na Mtoto wa mikoa mbalimbali kwa lengo la kutoa elimu kwa vijana balehe wengi ili kuboresha malezi katika familia na Taifa.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Msaidizi, Idara ya Mtoto kutoka Wizara hiyo Asha Shame wakati akifungua mafunzo ya siku tatu yanayofanyika katika mikoa ya Morogoro, Singida na Dodoma iliyoanza Oktoba 07-10, 2024.

Asha amesema Wizara itaendelea kutoa elimu hiyo itakayochochea mabadiliko ya fikra za wazazi na walezi katika kujenga jamii ya watoto wenye malezi bora, maadili na wenye tija kwa maendeleo ya taifa kwani elimu ya malezi inaanza kwenye familia ambapo familia ni chanzo cha Jamii yeyote ile duniani.

“Niseme lengo kuu la mafunzo haya ni kujengeana uwezo kuhusu elimu ya malezi na uzazi kwa vijana belehe. Tunafahau kuwa Familia ni chimbuko la tabia, mwelekeo na mtazamo wa mtu binafsi na jamii kwa ujumla katika maendeleo ya kijamii, kiutamaduni na kiuchumi. Vile vile, familia ni chimbuko la maadili ya kitaifa na uzalendo katika kudumisha umoja, amani na mshikamano,” amesema Asha.

Ameeleza Mwongozo wa Wajibu wa Wazazi/Walezi katika malezi na Matunzo ya Watoto na Familia ni jawabu la changamoto za malezi ya watoto zilizoibuliwa kupitia tafiti shirikishi kati ya wadau wa malezi iliyofanyika mwaka 2015 ambapo ilibainika wazazi wengi hasa wa kiume wamekuwa hawawajibiki kwenye malezi ya watoto na kupelekea jukumu hilo kubebwa na wazazi wa kike katika maeneo yote ya mjini na vijijini.

Aidha, amesema baada ya mafunzo hayo wawezeshwaji watakuwa na uwezo wa kupata mbinu mbalimbali zitakazowawezesha kufikia jamii kuanzia ngazi ya kaya pamoja na wadau muhimu katika malezi ya watoto wakiwemo viongozi wa dini, wazee wa mila na vyombo vya habari; Kupata elimu ya mnyororo chanya wa malezi ya watoto kuanzia kipindi cha utungaji wa mimba mpaka vijana balehe kupitia nguzo kuu tatu zilizoainishwa kupitia Mwongozo wa Wajibu wa Wazazi na Walezi katika Matunzo ya watoto na Familia ambazo ni Jali, Linda na Zungumza Naye.

Kwa upande wake Afisa Maendeleo ya Jamii Mkuu kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Victor Rugalabamu akiwasilisha mada katika mafunzo hayo kuhusu Kampeni ya Familia Bora Taifa Imara amesema, familia zimekuwa zikikumbana na changamoto nyingi katika malezi na matunzo ya watoto na familia ikiwemo hali ya umaskini, matumizi mabaya ya teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA), mwingiliano wa mila na desturi za mataifa mbalimbali ambazo baadhi zimechangia mmomonyoko wa maadili tunaoshuhudia.

Nao baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo kutoka mikoa ya Morogoro, Dodoma na Singida wamesema mafunzo hayo ni muhimu sana kwa ajili ya kutoa elimu kwa jamii hasa kwa wazazi/walezi, watoto na vijana balehe ili kuokoa kizazi ambacho kwa nyakati hizi kimekubwa na changamoto katika malezi ambazo husababisha mmomonyoko wa maadili kwa watoto na vijana hivyo elimu ikitolewa itasaidia kuboresha malezi na ustawi wa watoto na vijana balehe

Na. WMJJWM Singida

Chapisha Maoni

0 Maoni