Tanzania itapata fursa zaidi ya
kuboresha sekta yake ya misitu inayochangia kwa sasa asilimia 4.2 ya Pato la
Taifa (GDP), kufuatia utayari wa Serikali ya Finland (Ufini) na wadau wengine
wa teknolojia nchini hapa kusaidiana katika nyanja za teknolojia za kisasa.
Hayo yamesemwa jana na
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, mara baada ya
kutembelea makampuni na vituo kadhaa vya teknolojia za misitu katika mji wa
Joensuun hapa Ufini unaosifika kuwa kitovu cha sekta ya misitu nchini hapa.
“Tumetembelea makampuni makubwa
duniani yaliyoko hapa kama Abounat, John Deere, Business Finland na Kitivo cha
Teknolojia za Misitu cha Chuo Kikuu Finland kiitwacho East Finland University,”
ameeleza Dkt. Abbasi.
Moja ya makampuni mengi ya teknolojia
za misitu yaliyojikita katika mji huu ni kampuni ya John Deere inayoongoza
duniani kwa kubuni, kutengeneza na kuuza mitambo mbalimbali ya kupandia, kukata
na kuvuna mazao ya misitu hususani mbao na mazao yake ili kuipa thamani sekta
hiyo kuwa ya kibiashara zaidi kutokana na uzoefu wa Finland.
Ufini ambayo imekuwa ikitekeleza
miradi mbalimbali ya kusaidia sekta ya misitu nchini Tanzania ukiwemo Mradi wa
Forvac uliomalizika hivi karibuni uliochagiza ajira 500,000 katika sekta hiyo,
sasa iko tayari kusaidia mradi mwingine mpya kuendeleza mageuzi hayo.
“Kutokana na uzoefu wa wenzetu katika
biashara ya sekta ya misitu tayari tumekubaliana na tunakamilisha taratibu za
kuanza mradi mwingine mpya ambapo Finland itaisaidia Tanzania Euro milioni 20
kuchagiza mageuzi zaidi kuifanya sekta ya misitu kuisaidia Tanzania,” aliongeza
Dkt. Abbasi.
Dkt. Abbasi ameongoza ujumbe wa
wataalamu ambao ni Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki, Dkt. Deusdedit Bwoyo
na Kamishna wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Prof. Dos Santos
Silayo.
Ufini ndio nchi inayoongoza Barani
Ulaya kwa kuwa na eneo lenye misitu mingi, sehemu kubwa (asilimia 60)
ikimilikiwa na sekta binafsi na asilimia nyingine inayobaki ikiwa chini ya umma
ikisimamiwa na kampuni binafsi ya Serikali ya Forestry LTD. Mapato ya Ufini kwa
mwaka 2022 kutoka sekta ya misitu yalifikia Euro Bilioni 20 (Zaidi ya TZS
Trilioni 60).
0 Maoni