Benki ya Dunia, imemchagua Mtanzania,
Dkt. Zarau Wendeline Kibwe, kuwa Mkurugenzi Mtendaji mpya wa Benki hiyo
atakayesimamia Kanda Namba Moja ya Afrika inayojumuisha nchi 22 ikiwemo
Tanzania, nafasi ambayo Tanzania imewahi kuihudumu miaka 54 iliyopita.
Uamuzi wa Dkt. Kibwe kuikwaa nafasi
hiyo nyeti katika Taasisi hiyo kubwa ya Fedha Duniani, umetangazwa katika
Mkutano wa Mwaka wa Kundi la Kwanza la Nchi za Afrika wa Benki ya Dunia,
uliofanyika Jijini Washington D.C, nchini Marekani ambapo Mikutano ya Mwaka ya
Shirika la Fedha Duniani IMF na Benki ya Dunia inafanyika.
Kabla ya kuchaguliwa kuwa Mkurugenzi
Mtendaji mpya wa Benki hiyo atakayesimamia Kanda Namba Moja ya Afrika, Dkt.
Kibwe alihudumu katika Ofisi hiyo ya Bodi kama Naibu Mkurugenzi Mtendaji,
Mshauri na Mshauri Mwandamizi kwa zaidi ya miaka saba, tangu mwaka 2017.
Akizungumza Jijini Washington D.C,
baada ya kutangazwa kuchukua nafasi hiyo, Dkt. Zarau Wendeline Kibwe amesema
kuwa ataitumia nafasi hiyo kusimamia uendeshaji wa Benki na Taasisi zake Pamoja
na kutetea Maslahi ya nchi katika Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya Dunia pamoja
na maslahi ya Kanda ya Afrika anayoisimamia ili kukuza maendeleo na uchumi wa
nchi hizo.
Akizungumza kwa niaba ya Serikali
katika Mkutano huo uliomtangaza Dk. Kibwe kuchukua nafasi hiyo, Waziri wa
Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, anayeongoza Ujumbe wa Tanzania katika
Mikutano hiyo ya Mwaka ya Shirika la Fedha la Kimataifa – IMF na Benki ya
Dunia, amesema kuwa hayo ni matokeo ya juhudi za Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, anavyoifungua nchi na kukuza
Diplomasia ya Kimataifa.
Dkt. Nchemba amempongeza Dkt. Kibwe
kwa kupata nafasi hiyo na kwamba kutokana na umahili wake katika masuala ya
uchumi na fedha, pamoja na uzoefu wake wa muda mrefu katika Ofisi hiyo,
anaamini kuwa maslahi ya nchi yataendelea kulindwa ipasavyo kwa manufaa ya
watanzania.
Dkt. Zarau Wendeline Kibwe ni mchumi
wa kitanzania ambaye hivi karibuni amechaguliwa kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa
Benki ya Dunia kwa Kanda Namba Moja ya Afrika inayojumuisha nchi za Botswana,
Burundi, Eritrea, Eswatini, Ethiopia, Gambia, Kenya, Lesotho, Liberia, Malawi,
Msumbiji, Namibia, Rwanda, Shelisheli, Sierra Leone, Somalia, Sudan Kusini,
Sudan, Tanzania, Uganda, Zambia, na Zimbabwe.
Kabla ya kujiunga na Ofisi ya Bodi,
Dkt Kibwe alihudumu kama Mchumi wa Benki ya Dunia kwa Tanzania ambapo katika
kipindi cha miaka 15 ya kazi yake, Dkt. Kibwe amehudumu katika Serikali ya
Jamhuri wa Muungano katika nafasi mbalimbali ikiwemo ya Mchambuzi Mwanadamizi
wa Sera (Ofisi ya Rais – Tume ya Mipango), Mhadhiri Msaidizi (Chuo Kikuu
Dodoma), Afisa Forodha Msaidizi (Mamlaka ya Mapato Tanzania), na Mhadhiri
Msaidizi (Chuo Cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere).
Dkt. Kibwe ana Shahada ya Uzamivu
(Ph.D.) katika Uchumi wa Maendeleo, Shahada ya Uzamili (MA) katika Uchumi wa
Maendeleo, na Shahada ya Umahiri katika Sera za Umma, zote kutoka Taasisi ya
Taifa ya Mafunzo ya Sera (GRIPS) huko Tokyo, Japani.
Alipata Shahada yake ya Kwanza ya
Sayansi katika Uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe kilichopo Morogoro,
Tanzania.
Na. Benny Mwaipaja- Washington D.C.
0 Maoni