Mkurugenzi wa Idara ya Habari
(Maelezo) na Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Thobias Makoba, amesema kuwa Idara
ya Habari (Maelezo) Tanzania Bara na Idara ya Habari (Maelezo) Zanzibar
zimedhamiria kuimarisha ushirikiano ili kuongeza ufanisi wa mawasiliano kati ya
Serikali na wananchi wa pande zote za Muungano.
Makoba ameeleza dhamira hiyo Oktoba
25, 2024 mjini Unguja, Zanzibar baadaa ya kufanya ziara katika ofisi za Idara
ya Habari (Maelezo) Zanzibar na kukutana na Kaimu Mkurugenzi wa Idara hiyo, Bi.
Asha Juma Khamis.
“Idara hizi mbili zina majukumu muhimu
sana katika kuratibu mawasiliano kati ya Serikali na wananchi, hivyo ni muhimu
kuimarisha ushirikiano wa ofisi hizi ili kuziwezesha kufanya kazi kwa ufanisi
katika usimamizi wa sekta ya habari nchini na katika kuratibu mawasiliano kati
ya Serikali na wananchi,” ameeleza Msemaji Mkuu wa Serikali.
Amesema ushirkiano huo utagusa maeneo
mbalimbali yakiwemo kubadilishana taarifa, kujenga uwezo wa watumishi pamoja na
mafunzo hususani katika teknolojia zinazoibukia na njia za kisasa za upashaji
habari ili kuzifanya idara hizo kufanya kazi kwa weledi hasa katika kipindi
ambacho dunia imekuwa na upotoshaji wa taarifa kutokana na kukua kwa teknolojia
ya habari na mawasiliano.
Aidha, Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw.
Thobias Makoba pamoja na mwenyeji wake, Kaimu Mkurugenzi wa Maelezo Zanzibar,
wametumia fursa hiyo kujadili maandalizi ya Kikao Kazi cha Maafisa Habari,
Mawasiliano na Uhusiano wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kinachotarajia kufanyika mwezi Macchi 2025.
Kwa upande wake, Bi. Asha Juma Khamis
ameelezwa kufurahishwa na ziara hiyo kwa sababu ushirikiano wa Idara hizo ni
kielelezo tosha cha namna Idara hizo zinavyotekeleza majukumu yake kwa manufaa
ya Serikali zote na wananchi kwa ujumla.
“Sisi kwetu ni faraja kubwa
kutembelewa na Msemaji Mkuu wa Serikali Bw, Makoba, kwani ni mara yake ya
kwanza kututembelea tangu ateuliwe mwezi Juni mwaka huu na ni imetupa hamasa na
ari mpya ya kuimarisha ushirikiano wetu,”ameeleza Asha.
Idara hizi zimekuwa na utamaduni wa
kushirikiana katika kutekeleza majukumu ya usimamizi wa sekta na kuzisemea
Serikali katika utekelezaji wa Sera, mipango na miradi mbalimbali ya maendeleo,
na pia kufanya ziara za kubadilishana uzoefu, mafunzo pamoja na kushiriki Vikao
Kazi mbalimbali vinavyoandaliwa na Idara hizo.
0 Maoni