Tamasha la Nyama Choma Mlima Hanang’ Lafana

 

Tamasha maarufu la Mt Hanang’ Nyama Choma Festival 2024 limefana kwa mara nyingine, likivutia watalii wa ndani zaidi ya 120 katika Hifadhi ya Mazingira Asilia ya Mlima Hanang’ iliyopo katika mji wa Katesh, mkoani Manyara.

Tamasha hili, ambalo linafanyika kila mwaka, lilifanyika msimu huu kuanzia tarehe 31 Agosti hadi 1 Septemba 2024, limewavuta wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini kutokana na Hifadhi hio kuwa ni kivutio cha kipekee kwa watalii wa ikolojia na utamaduni.

Mratibu wa Tamasha Hilo na Afisa Utalii wa Mt Hanang’, Elizaberth Mbunda amesema tamasha hilo lenye lengo la kutangaza vivutio vya kitalii ndani ya hifadhi hiyo limekuwa likizidi kupata umaarufu mkubwa kutokana na uwepo wa maeneo mbalimbali ya kitamaduni, kihistoria na urithi kama vile maeneo matakatifu ya jamii za Wabarabaig na maziwa ya soda ya Balang'dalalu na Gendabi.

“Mlima Hanang' ni eneo maarufu kwa mazoezi ya kupanda Mlima Kilimanjaro lakini pia una mandhari za kuvutia, sasa ili kukuza shughuli za utalii tumeamua kuja na nyama choma festival ambapo washiriki walipata fursa ya kutembelea maeneo mbalimbali ya kuvutia kama vile msitu mnene, maporomoko ya maji, na sehemu za matazamio za "viewpoint" ambapo walishuhudia mawio na machweo ya jua na kisha kufurahia kwa kula nyama choma zilizoambatana na burudani mbalimbali za usiku, ikiwemo camping, kuota moto, na muziki,” anasema.

Aidha, amesema kuwa hali ya utalii imeendelea kuwa shwari licha ya athari zilizowahi kusababishwa na maporomoko ya maji hapo awali.

Kwaniaba ya Mkuu wa Wilaya Ndugu Athumani Likeyekeye katibu tawala wilaya ya Hanang aliipongeza TFS kwa kuendelea kuboresha utalii katika Hifadhi ya Mlima Hanang’.

Kamanda wa Kanda ya kati – TFS, Kamishna Msaidizi mwandamizi Mathew Kiondo ni miongoni mwa viongozi walishiriki tamasha hilo “niwapongeze waandaaji kwa ubunifu wao na kuendeleza uhamasishaji wa wananchi kuja kujionea shughuli za utalii ikolojia ndani ya Hifadhi ya Mlima Hanang’.

Hifadhi ya Misitu ya Asili ya Mlima Hanang' ina eneo la hekta 5,871 katika kimo kinachotofautiana kati ya mita 1860 hadi 3423 juu ya usawa wa Bahari. Mlima Hanang’ ni mlima wa nne kwa urefu nchini Tanzania baada ya Kilimanjaro, Meru, na Lolmalasin ukiwa na kimo cha mita 3423 juu ya usawa wa bahari.

Hifadhi ya Misitu ya Asili ya Mlima Hanang' ina shughuli nyingi za kiikolojia na kiutamaduni kama vile ngoma za jadi, mapambo ya kitamaduni, kutembelea maeneo matakatifu, kuonja pombe za kienyeji, kupanda mlima na kufuatilia njia, kutazama wanyamapori, kutazama ndege, matembezi ya msituni na upigaji picha. Pia, kuna fursa ya kutazama Bonde la Ufa na mapango unavyopanda kuelekea kilele cha Mlima Hanang'.



Chapisha Maoni

0 Maoni