Katika kisiwa kidogo cha Rukuba kilichoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Musoma Vijijini, Mkoani Mara maisha ya wananchi sasa yanaonekana kuwa na mwangaza mpya.
Hadi hivi karibuni, wakazi wa kisiwa hiki walikuwa
wakipambana na adha kubwa ya usafiri kwa boti ili kuwapeleka wagonjwa wao kwa
huduma za upasuaji mdogo nje ya kisiwa hicho. Hali hiyo ilikuwa kero kubwa,
hasa wanawake walipokuwa wanahitaji upasuaji wa dharura.
Kisiwa cha Rukuba, kilichopandishwa hadhi kuwa kijiji mnamo
mwaka 1974, kilikuwa kinategemea huduma ya Zahabati, na wagonjwa walilazimika
kusafiri kwa boti kwa muda mrefu ili kufika hospitalini. Safari hii ilikuwa ni
ngumu na yenye hatari, hasa kwa wagonjwa waliokuwa na hali mbaya.
Hata hivyo, mabadiliko makubwa yamekuja baada ya serikali
kutekeleza mradi wa kujenga Kituo cha Afya chenye umeme jua. Rais Samia Suluhu
Hassan, akiungana na mbunge wa Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo,
walishughulikia ujenzi wa kituo hiki kwa gharama ya shilingi milioni 500 na
vifaa tiba vilivyogharimu shilingi milioni 100.
Wakazi wa Rukuba sasa wanaweza kusema kwamba maisha yao
yameimarika. Hassan Juma Ibrahim, mmoja wa wakazi wa kisiwa hicho, alieleza
furaha yake kwa kusema, "Mbunge wetu amefanya kazi kubwa sana,
amefanikisha kutuletea shilingi milioni 345 kwa ajili ya umeme jua wa mradi wa REA.
Umeme huu utawezesha wagonjwa kupata huduma za matibabu nyakati za usiku bila
shida yoyote."
Abdalah Suma aliongeza kwa kusema, "Awali ilikuwa
vigumu sana wakati mama alihitaji upasuaji mdogo wa dharura. Lakini sasa, umeme
jua utaondoa matatizo yote hayo. Hii ni neema kwa sekta ya afya na pia kwa
elimu, kwani umeme huu utatumika katika taasisi za elimu pia."
Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Chama cha Mapinduzi (CCM)
Wilaya ya Musoma, Thomas Kipango, alieleza jinsi kituo hicho kilivyokuwa msaada
mkubwa kwa jamii. "Tulikuwa tunakabiliwa na ugumu wa kusafirisha wagonjwa
kwa boti, ambapo mara nyingine ilikuwa inachukua zaidi ya saa moja na nusu
kabla ya kufika matibabu. Sasa, adha hiyo imekwisha," alisema Kipango.
Kisiwa cha Rukuba, ambacho kinategemea uvuvi kama chanzo kikuu cha uchumi, kimepata suluhu ya huduma bora za afya na umeme jua, na hivyo kuifanya jamii yake kuwa na matumaini mapya.
0 Maoni