Hifadhi ya Amani kuwa kivutio kikuu cha utalii nchini

 

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii anayesimamia Utalii, Nkoba Mabula, ametembelea Hifadhi ya Mazingira Asilia Amani na kuonyesha matumaini makubwa juu ya uwezo wa hifadhi hiyo kuwa kivutio kikuu cha utalii nchini, akifananisha na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

Mabula alisisitiza kuwa hadithi za bioanuwai na mandhari yake zinathibitisha kuwa, ikitangazwa vyema, hifadhi hiyo inaweza kuvutia watalii wengi na kuchangia pato la taifa.

Akizungumza baada ya kutembelea hifadhi hiyo Septemba 25, 2024, Mabula aliongeza kuwa hifadhi hiyo inatoa fursa kubwa kwa utalii wa kiikolojia na inapaswa kupewa kipaumbele katika mipango ya maendeleo ya sekta ya utalii. “Kutembea katika Hifadhi ya Amani ni kama kuwa katika bustani ya furaha na amani. Uzuri wa asili na utulivu wake, pamoja na sauti za ndege adimu, vinachangia sifa yake ya kipekee,” anasema.

Mabula alivutiwa kusikia kuwa hifadhi hiyo, iliyoko katika wilaya za Muheza na Korogwe mkoani Tanga, ni makazi ya maua maarufu ya "African Violet" (Saintpaulia), ambayo yana umuhimu wa kiikolojia na kiroho, hasa katika kuhamasisha nguvu ya msamaha.

Alphonce Nyululu, Mhifadhi wa Hifadhi ya Mazingira Asilia Amani, alisema hifadhi hiyo iliyoanzishwa mwaka 1997 inajulikana kama moja ya maeneo 12 bora duniani kwa utazamaji wa ndege, na imeorodheshwa na UNESCO kama sehemu ya Hifadhi za Maisha na Mazingira Duniani.

Someni Mteleka, Mkuu wa Kitengo cha Utalii, aliongeza kuwa mapato ya hifadhi hiyo yameongezeka kutokana na upekee wa rasilimali zake na urahisi wa kufikika, huku maboresho ya miundombinu yaliyofadhiliwa na mradi wa UVIKO-19 yakiwavutia watalii wengi zaidi.

Kamanda wa Uhifadhi wa Kanda ya Kaskazini, James Nshare, alishukuru kwa ziara ya Mabula, akisema imetoa motisha zaidi ya kukuza utalii wa hifadhi hiyo na kuahidi kuendeleza juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania.



Chapisha Maoni

0 Maoni