Mitambo ya Maji Bukanga, Musoma Mjini kumaliza adha ya maji

 

Katika juhudi za kuboresha upatikanaji wa maji safi, mitambo iliyofungwa Bukanga, Musoma Mjini inazalisha lita milioni 36 za maji kwa siku, kiasi ambacho ni kikubwa kuliko mahitaji ya kila siku ya Mji wa Musoma, uliopo mkoani Mara.

Ili kuimarisha usambazaji wa maji, tenki kubwa lenye ujazo wa lita milioni tatu limejengwa Mlimani Bharima, na MUWASA wanaendelea kusambaza maji ya bomba katika jimbo la Musoma Vijijini.

Taaifa ya Mbunge wa Musoma Vijijini Prof. Sospeter Muhongo imesema tenki hilo litatumika kusambaza maji ya bomba ndani na nje ya Mji wa Musoma. Serikali imeipa MUWASA jukumu la kusambaza maji haya kwa vijiji jirani, ikiwemo vijiji vya Musoma Vijijini na Butiama.

MUWASA imepanga kusambaza maji kwenye kata nne za Musoma Vijijini, kwenye Kata ya Etaro vijiji vitatu, Kata ya Nyegina vijiji vitatu, kata ya Nyakatende vijiji vinne na Kata ya Ifulifu vijiji vitatu.

Taarifa inasema hadi sasa, usambazaji wa maji ya bomba umefanikiwa kwenye baadhi ya vijiji vya Kata ya Etaro (Busamba, Etaro, na Mmahare) na Nyegina (kijiji cha Mkirira) ambapo kazi yakutandaza bomba kuu kuelekea Nyegina Senta inaendelea.

Aidha, imeeleza taarifa hiyo kuwa katika Jimbo la Musoma Vijijini, vijiji 68 vinanufaika na miradi ya maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria, ambapo vijiji 53 kati ya 68 (77.94%) tayari vinatumia maji ya bomba.

Miradi mingine ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji, na baadhi ya vijiji vinafanyiwa kazi ya kuchimba visima virefu, hasa katika Kata ya Bugwema. Kazi hii inafanywa kwa ushirikiano kati ya RUWASA, MUWASA, na BADEA. 

Wananchi wa Jimbo la Musoma Vijijini na viongozi wao wote wameendelea kuishukuru Serikali chini ya uongozi mzuri wa Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutupatia fedha nyingi za kutekeleza miradi ya maendeleo kwenye vijijini vyao, ikiwemo miradi ya maji safi na salama ya bomba, imemalizia taarifa hiyo.

Chapisha Maoni

0 Maoni