TFS pungezeni kutoa vibali vya kukata miti kwa ajili ya kuchoma mkaa

 

Watumishi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania(TFS) Mkoa wa Dodoma wametakiwa kupunguza kutoa vibali vya kukata miti kwaajili ya kuchoma Mkaa kwani Nishati ya Mkaa inachangia kwa kiasi kikubwa kwenye uharibifu wa mazingira na hivyo kudhoofisha juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali za kupambana na mabadiliko ya tabia nchi.

Haya yamesemwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dr. Philip Isdor Mpango akiwa kwenye ziara ya siku tatu ya mkoa wa Dodoma ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika mkoa huo. Aidha Mhe. Mpango amewaasa Wananchi wa Wilaya za Chamwino na Bahi kuacha kuharibu mazingira kwa kukata miti hovyo pamoja na kutoharibu maeneo oevu ambayo mengi ni vyanzo vya maji.

Mhe. Mpango ameelekeza elimu itolewe kwa wananchi ili waweze kutumia nishatI safi ambayo ni mbadala kwa ajili ya kupikia na kusisitiza utunzaji wa mazingira kwa kupanda miti kwa wingi ili kupunguza changamoto ya mabadiliko ya tabia nchini.

Katika ziara hiyo Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Pindi Hazara Chana amewakilishwa na Naibu Wazili wa Maliasili na Utalii Mhe. Dunstan Kitandula.

Mhe. Kitandula alipopewa nafasi ya kusalimia wananchi alisema kuwa Wizara ya Maliasili itaendelea kusimamia na kulinda maliasili zilizopo nchini sambamba na kuwalinda wananchi wanaokabiliwa na changamoto ya wanyama wakali na waharibifu.

Vilevile Mhe. Kitandula aliongeza kuwa wizara Itaendelea kupambana na changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi kwa kuhimiza utunzaji wa misitu na upandaji wa miti kwenye maeneo yaliyo athirika kutokana na uharibifu wa mazingira.

Na. Anangisye Mwateba- Dodoma

Chapisha Maoni

0 Maoni