Muhimbili kuendelea kuboresha huduma za upasuaji rekebishi

 

Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Prof.Mohamed Janabi amekutana na Afisa Mkuu kutoka Shirika lisilo la Kiserikali la Marekani ReSurge International kwa lengo la kuendeleza ushirikiano na kujengeana uwezo katika kufanya upasuaji rekebishi kwa watu wenye changamoto mbalimbali ikiwemo waliopata ajali ya kuungua moto na wenye misuli iliyokakamaa kutokana na majeraha.

Akizungumza wakati wa kikao hicho Prof. Janabi amesema Muhimbili ina nguzo tatu muhimu ambazo ni Huduma, Elimu na Utafiti hivyo kama Hospitali ya Taifa haina budi kutekeleza kwa vitendo kwakuwa ni wajibu wetu.

Ameeleza kuwa MNH itaendelea kuboresha ushirikiano na wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi ili kuendelea kuwajengea uwezo wataalam wake zaidi katika kutoa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi hapa nchini.

“Ili kuendena na mabadiliko ya sayansi na teknolojia katika tiba, naamini katika kujifunza na kuongeza elimu kwa kubadilishana uzoefu kutoka kwa watua ambao wanajua zaidi,” amesema Prof. Janabi.

Kwa upande wake, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa MNH, Dkt. Ibrahim Mkoma, amesema mwanzoni mwa mwaka huu MNH ilishirikiana na wataalam kutoka shirika hilo na kufanya kambi maalum ya siku tano iliyohusisha upasuaji wa urembo na upasuaji wa matibabu (Cosmetic and Reconstructive Surgery) kwa wagonjwa nane.

Chapisha Maoni

0 Maoni