Wadau wa utalii duniani wavutiwa kuwekeza Tanzania

 

Kampuni kubwa zinazojishughulisha na masuala ya utalii duniani zimevutiwa kuwekeza nchini Tanzania katika huduma za malazi, usafirishaji na  utangazaji utalii.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) katika Maonesho ya Utalii ya ITB yanayoendelea jijini Berlin Ujerumani.

“Nimefurahi kukutana na kampuni kubwa ya TUI (TUI Group) yenye Makao Makuu nchini Ujerumani ambayo ina hoteli zaidi ya 400 duniani, meli za kitalii 16, mashirika ya ndege matano na zaidi Mashirika 1,200 ya usafiri,” Mhe. Kairuki amesisitiza.

 Amefafanua kuwa kampuni hiyo imewekeza Zanzibar na hadi kufikia mwezi Juni mwaka huu itazindua hoteli yao ya tisa lakini kwa upande wa Tanzania Bara inaendelea kufungua safari za ndege ili kuleta watalii katika hifadhi zilizopo nchini Tanzania.

 Waziri Kairuki ametumia fursa hiyo kuihamasisha kampuni hiyo ili iongeze uwekezaji kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara katika huduma za hoteli, ndege za kukodi kwa lengo la kuhakikisha Tanzania ina ndege nyingi zaidi za kwenda maeneo mbalimbali ya vivutio vya utalii.

“Tumewaomba waendelee kushirikiana na sisi kama Serikali katika kutangaza utalii wa Tanzania katika ndege zao,hoteli zao na tuweze kufanya kampeni mbalimbali za kutangaza utalii kwa pamoja,” Waziri Kairuki amesema.

Aidha, Mhe. Kairuki amekutana na kampuni inayosafirisha watalii zaidi ya milioni 1.2 duniani yenye Makao Makuu  Marekani  na Puertoriko ambayo imeonyesha utayari na kuanzia mwezi Mei mwaka 2024 italeta Wakala wa Usafirishaji zaidi ya 40 kutembelea maeneo mbalimbali nchini Tanzania.

Waziri Kairuki pia amekutana na kufanya mazungumzo na Kampuni ya Kimataifa ya Utangazaji ya Expedia Group pamoja na kampuni kutoka Slovakia ambayo inapeleka watalii duniani kwa zaidi ya asilimia 85 kutoka nchini humo na ina matangazo katika luninga zao na kujadili namna ya kushirikiana katika kuandaa matangazo ya vivutio vya utalii.

Vilevile Mhe. Kairuki amekutana na Wadau wa usafirishaji watalii wenye ulemavu kutoka nchini Afrika Kusini kuona namna bora ya kutengeneza vifurushi (package) vya kutalii kwa ajili ya watu wenye ulemavu kutembelea nchini Tanzania.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Damas Mfugale amesema ushiriki wa Tanzania kwenye Maonesho hayo ni chachu ya kuongeza idadi ya watalii nchini.

Naye, Mmoja wa Washiriki kutoka nchini Tanzania ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya African Qeen Adventures, Alice Manupa amemshukuru Rais Samia kwa kuwa Royal Tour imeweza kuitangaza Tanzania kimataifa.

Na. Mwandishi Wetu-Berlin


Chapisha Maoni

0 Maoni