Muhimbili kuhifadhi historia ya sekta ya afya nchini

 

Mkurugenzu Mkuu wa Makumbusho ya Taifa la Tanzania, Dkt. Noel Lwoga pamoja na wataalamu wake wamekutana na Mkurugenzi Mkuu wa Hospital ya Taifa ya Muhimbili, Prof. Mohamed Janabi kwa lengo la kujadili namna bora ya kuhifadhi Historia ya Sekta ya Afya na Hospital ya Taifa Muhimbili sambamba na maendeleo ya Sekta ya Afya nchini.

Viongozi hao  wamekutana leo katika hospitali hiyo kwa lengo la kuangalia namna bora ya kushirikiana katika utekelezaji wa jambo hilo kabla ya ujenzi wa majengo mapya kuanza ambapo maandalizi ya utunzaji wa historia ya hospitali hiyo tangu enzi za Sewahaji hadi sasa.

Mkurugenzi Mtendaji wa MNH Prof. Mohamed Janabi amemueleza Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa, Dkt. Noel Lwoga kuwa, upembuzi yakinifu kuhusu mradi huo unaratajia kuanza mapema mwaka 2024 ambapo katika ujenzi huo, utunzaji historia ni kipaumbele namba moja, baadhi ya majengo yatabaki na mojawapo litakuwa makumbusho ili kulinda historia yake kwa vizazi vijavyo kuhusu hatua moja hadi nyingine ambazo Taifa limepitia katika maboresho ya utoaji huduma katika sekta ya afya nchini.

“Hospitali ina majengo mengi ya zamani, yanayohitaji ukarabati mkubwa na kutokukidhi mahitaji ya sasa ya utoaji huduma hivyo tunahitaji kuijenga upya, katika hilo tutazingatia mambo mengi ikiwemo kuweka huduma karibu ili kupunguza usumbufu kwa wagonjwa kutembea mita 500 kufuata kipimo flani au huduma nyingine sehemu flani” amesisitiza Prof. Janabi.

Amesema, ujenzi huu utazingatia matumizi sahihi ya ardhi ambapo eneo kubwa litakuwa wazi baada ya ujenzi huo kwani majengo yatakuwa machache ukilinganisha na hali ilivyo sasa, kutakuwa na ramani moja (comprehensive plan), kukidhi vigezo vingi vya kimataita vya utoaji huduma, kuboresha na kuongeza huduma za kibobezi, kuwa kituo cha mafunzo ya huduma za ubobezi na kuifanya Hospitali kuwa kituo cha Utalii Tiba (Medical Tourism Hub).

 Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa, Dkt. Lwoga ameipongeza Menejimenti ya hospitali kwa kutambua umuhimu wa kuhifadhi historia ya taifa kwa ajili ya vizazi vijavyo na kuahidi kutoa ushirikiano wa hali ya juu kutimiza azma hiyo.

Chapisha Maoni

0 Maoni