Kampeni ya Mpanga/Kipengere Uni Retreat yazaa matunda

 

Kampeni ya kuhamasisha wanafunzi wa vyuo vikuu kutembelea Hifadhi ya Mpanga Kipengere iliyopo Mikoa ya Njombe na Mbeya ijulikanayo kwa jina la "Mpanga/Kipengere Uni Retreat" imeanza kuonesha matokeo makubwa kwa wanavyuo mbalimbali kuanza kutembelea Hifadhi hiyo.

Kampeni hiyo iliyozinduliwa Desemba 6, 2023 na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania - TAWA kupitia Pori la Akiba Mpanga/Kipengere kwa kushirikiana na Chikanda Safaris & Adventure ilikuwa na lengo mahsusi la kuwahamasisha wanafunzi wa vyuo vikuu nchini hususan vya Kanda ya Nyanda za Juu kusini kutembelea Hifadhi hiyo ili kujionea vivutio mbalimbali vya kitalii, maajabu yaliyopo na kujifunza mengi kuhusu historia adhimu iliyo ndani ya Hifadhi hiyo

Katika kuonesha mwitikio,  Desemba 17, 2023 Hifadhi ya Mpanga Kipengere ilipokea kundi la kwanza la wanafunzi wapatao 31 kutoka vyuo mbalimbali waliotembelea hifadhi hiyo

Akizungumza wakati wa mapokezi ya wanafunzi hao ndani ya hifadhi hiyo, Kamanda wa Hifadhi ya Mpanga/Kipengere Donasian Makoi alisema hifadhi ya Mpanga/Kipengere ina utajiri wa kipekee wa idadi kubwa ya maporomoko ya maji yenye muonekano adhimu lakini pia pango la Chifu Mkwawa na eneo la uoto wa asili lenye maua ya kipekee lijulikanalo kwa jina la ibaga mambo ambayo yangeweza kuwa kivutio kikubwa katika safari yao ya Utalii.

TAWA kwa kushirikiana na Chikanda Safaris inaendelea kuwahamasisha watanzania wote kutembelea Hifadhi ya Mpanga/Kipengere hasa katika kipindi hiki cha msimu wa Sikukuu za Christmas na Mwaka Mpya.

Na. Beatus Maganja

Chapisha Maoni

0 Maoni