Bodi na Menejimenti ya
Huduma za Meli nchini (MSCL) wametakiwa kusimamia kikamilifu miradi
inayotekelezwa na serikali ili kuhakikisha fedha iliyotolewa kwa ujenzi inaleta
thamani.
Maagizo hayo yametolewa
Jijini Mwanza na Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile katika hafla ya
utiaji saini mikataba ya ukarabati wa meli tatu zitakazogharimu shilingi bilioni
48.092 pamoja na uzidunzi wa meli ya Mv Umoja iliyogharimu shilingi bilioni 21.
Naibu Waziri Kihenzile
amesema kusainiwa kwa miradi hiyo mitatu kunalenga kukidhi mahitaji ya usafiri kwa
abiria hususani katika Ziwa Tanganyika na kutumia fursa zilizopo katika kuhudumia
masoko ya nchi jirani.
"Ukarabati wa meli ya
kubeba abiria na mizigo ya MV Liembe itasaidia kurejesha huduma ya usafiri wa
abiria na mizigo, meli MT Nyangumi itasaidia usafirishaji wa shehena ya mafuta
kuelekea nchi ya Uganda na Sudan ya Kusini, pamoja na Meli ya MT Ukerewe
itakuwa ni msaada mkubwa kwa ajili ya shughuli za uokozi katika ziwa Victoria
wakati wa dharura," amesema Kihenzile.
Amefafanua kuwa ukarabati wa
meli hizo utawasaidia wakazi wa mwambao wa Ziwa Tanganyika pamoja na nchi za
jirani za DRC, Burundi na Zambia, hivyo na serikali imeweza kuonesha kuwa
wameanza kuleta mapinduzi katika sekta ya usafiri kwa njia ya maji.
Kwa upande wake Mkuu wa
Wilaya ya Nyamagana Amina Makilagi akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Amos
Makalla ameeleza kuwa usafiri wa njia ya maji ni tegemeo kwa wakazi wa Kanda ya
Ziwa na ni kichocheo kikubwa kwa wananchi wa ukanda huo katika kukuza uchumi.
Makilagi amefafanua kuwa
ujio wa meli hiyo ya MV Umoja itakuwa ni chachu kwa Watanzania pamoja na kuleta
matokeo chanya yenye tija katika kukuza uchumi wa Mkoa wa Mwanza na ukanda wa
ziwa Victoria na Taifa kwa ujumla.
"Hii inatokana na
usafiri wa meli kuwa na bei rahisi ya usafiri ukilinganisha na usafiri mwingine
wote ni mashahidi kwa wale tunaosafiri," amesema Makilagi.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Huduma
za Meli (MSCL) Eric Hamis amesema meli ya MV Umoja kabla ya ukarabati ilikuwa
inabeba mabehewa 19 na baada ya ukarabati inauwezo wa kubeba mabehewa 22 na
tani 1200 ya mizigo.
"Meli hii tayari
imeanza kutoa huduma kati ya Mwanza na Bandari za Uganda na hivyo kufungua
usafirishaji wa shehena ya mizigokupitia ushiroba wa kati kuelekea Nchini
Uganda na Sudan ya kusini," alisema Hamis.
Meli ya kubeba mizigo ya MV
Umoja inayobeba shehena ya mizigo katika Ziwa Victoria imefanyiwa ukarabati
mkubwa uliogharimu kiasi cha dola za Marekani 8,422,840 ambazo ni sawa na sh,
19,811,446,192 za Tanzania.
0 Maoni