Tanzania yaanza maandalizi ushiriki Mining Indaba 2024

 

Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa kushirikiana na Wadau wa Sekta ya Madini imeanza maandalizi ya kushiriki Maonesho Makubwa ya Madini Barani Afrika ya Mining Indaba.

Maonesho hayo yatakayofanyika mwezi Februari 2024, katika jiji la Cape Town nchini Afrika Kusini yatashirikisha wafanyabiashara, watoa huduma, taasisi mbalimbali za kisekta pamoja na wakuu wa kampuni kubwa za uchimbaji madini duniani.

Akizungumza wakati akiwasilisha mpango wa ushiriki wa Tanzania katika Maonesho hayo kwa Waziri wa Madini kwa niaba ya Sekretarieti ya maandalizi, Mwenyekiti wa Chemba ya Migodi Mhandisi Philbert Rweyemamu amesema ni moja ya maonesho ambayo huwakutanisha wawekezaji wapatao angalau 900, taasisi za sekta zipatazo angalau 40 na watendaji wa kampuni wapato 1000.

Akizungumza katika kikao hicho, Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde amesema ushiriki watanzania Katika Maonesho hayo unatarajia kuiweka Tanzania kwenye ramani ya Afrika na dunia nzima huku ukileta sauti moja kwa wadau kuielewa Tanzania.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara ya Madini Kheri Mahimbali amesema dhamira ya Wizara ni kuweka ushiriki wa pamoja katika banda moja la wizara, taasisi na wadau ili kufanya ushiriki wenye tija zaidi kwa Tanzania.

Tanzania inatarajia kutumia maonesho ya Mining Indaba kuvutia mitaji, uwekezaji, kujifunza, kuleta teknolojia bora za uchimbaji, kujenga mahusiano ya kibiashara, kuimarisha ushirikiano pamoja na mambo mengine.

Kampuni zinazotarajia kudhamini ushiriki wa Tanzania katika maonesho hayo ni pamoja na Anglo Gold Ashanti, Barrick Gold, Shanta Gold, Mantra Tanzania, Tembo Nickel, TRX Gold, Petra Diamond na City Engineering Ltd.

 #TanzaniaItakuwepo#

#MiningIndaba2024#

VISION 2030: Madini ni Maisha na Utajiri

Chapisha Maoni

0 Maoni