TAWA yakabidhiwa cheti cha shukrani kwa wadhamini wa S!TE

 

Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Angellah Kairuki amekabidhi cheti cha shukrani kwa wadhamini wa maonesho ya Saba ya Kimataifa ya Swahili International Tourism Expo - S!TE kwa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) na  kutambua mchango wake katika kudhamini  na kuwa sehemu ya mafanikio ya maonesho hayo ambayo yalifana kwa kiwango kikubwa.

TAWA ni miongoni mwa mashirika na Taasisi za Serikali zilizojitokeza kushiriki na kudhamini maonesho haya ya Kimataifa ya Utalii yaliyofanyika Mlimani City Jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 6 - 8 Oktoba, 2023 ambapo kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA Mabula Misungwi Nyanda, cheti hicho kimepokelewa na Mhifadhi Mwandamizi - Utalii Steven Madenge

Akifunga rasmi maonesho hayo kwa mwaka 2023, Waziri Kairuki amewashukuru wote waliohudhuria na kushiriki katika maonesho haya lakini kipekee amewashukuru TAWA kwa kuwapeleka Wanyamapori hai katika maonesho hayo ambao kwa kiasi kikubwa wamechagiza na kuleta vionjo vya aina yake na ladha ya kipekee katika maonesho hayo

"Niwashukuru kwa mara nyingine tena wote kwa kuhushuria katika maonesho haya muhimu kwa Taifa letu lakini vilevile katika sekta hii ya utalii, katika biashara ya utalii na uwekezaji wa utalii," amesema waziri Kairuki.

"Niwashukuru pia TAWA kwa kuleta Wanyamapori hai naamini kwa walioweza kutembelea mabanda hayo ya TAWA wameweza kufurahia bustani ya Wanyamapori hao," ameongeza Mhe. Kairuki

Aidha, Waziri Kairuki amewakaribisha tena wadau wote katika S!TE 2024 inayotarajiwa kufanyika tarehe 11 - 13 Oktoba 2024.

Na. Beatus Maganja- Dar es Salaam

Chapisha Maoni

0 Maoni