Rekodi mpya imeandikwa
katika Hifadhi ya Taifa Tarangire iliyopo mkoani Manyara baada ya
kupokea watalii wa ndani zaidi ya 700 waliotembelea hifadhi hiyo inayosifika
Tanzania kwa kuwa na makundi makubwa ya Tembo.
Watalii hao wa ndani waliotoka katika Chama cha Wafanyakazi
wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE), wameingia leo tarehe 26.10.2023 wakiwa
katika magari (Cruzer - Warbus) 108 yaliyokuwa yakiongozana mithili ya msafara
wa Mfalme akiingia katika Kasri yake.
Umuhimu wa idadi hii ya watalii wa ndani, hautainufaisha
Hifadhi ya Taifa Tarangire tu, bali itaongeza mzunguko wa fedha katika vijiji
vya Minjingu, Kakoi na Olevolosi kwa manunuzi ya mahitaji muhimu watakayofanya
wakati wa ziara hiyo.
Mwenyekiti wa TUGHE Taifa, Ndg. Joel Kamunyoge aliyeongoza
kundi la watalii hao alisema kuwa ujio wao umetokana na wito uliotolewa na Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan, wa kuwataka
Watanzania kuvipenda, kuvithamini na kuvitembelea vivutio vya utalii vilivyoko
nchini Tanzania.
"Sisi TUGHE ni desturi yetu kila tunapomaliza vikao
vyetu vya kila mwaka, kutembelea maeneo yanayochangia uchumi kwa taifa na
katika ziara hii tumeona ni vyema kuungana na Rais wetu Dkt. Samia kutangaza
utalii wa ndani na kuchangia pato la taifa kwa viingilio tulivyotoa."
Naye, Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Hery Mkunda, amelipongeza
Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kwa kuboresha miundombinu ya
barabara na sehemu za mapumziko zinazotumika kwa ajili ya kupata chakula
"Picnic sites."
"Sikutarajia kwa idadi yetu hii, kama tungeweza kutalii
kwa uhuru na bila msongamano, lakini tumeshangaa kuona barabara nyingi na nzuri
zilizotuwezesha kuona wanyama wengi na kwa ukaribu zaidi", aliongeza
Mkunda.
Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Beatrice Kessy, alisema
kuwa hifadhi hiyo leo imeweka rekodi mpya ya kupokea idadi kubwa zaidi ya
watalii wa ndani tangu kuanzishwa kwake 1970. "Idadi hii inatupa matumaini
kama shirika kuongeza kasi ya kutangaza vivutio vyetu."
"Tunawapongeza sana watanzania wenzetu kutoka TUGHE kwa
kuona umuhimu wa kutembelea vivutio vya utalii nchini, pia kwa kuichagua
Hifadhi ya Taifa Tarangire kwa mwaka
huu, hivyo ni rai yetu kama shirika kuwaomba watanzania wengine kuiga mfano wa
TUGHE," aliongeza Kamishna huyo.
Naye, Mkurugenzi wa kampuni ya utalii ya Tanzanite Corporate
Limited Elina Benson Mwangomo, aliishukuru Serikali kwa kuendelea kuleta vikao
Arusha, kwani imekuwa ni fursa kwake na timu yake kupata watalii hao.
"Vikao hivi vimekuwa ni fursa kwetu vijana kujipatia
kipato kwa kuwatembeza watalii hawa katika Hifadhi ya Taifa Tarangire, pia
kikubwa zaidi nawashukuru TANAPA kwa sababu haikuwa rahisi kwa kampuni peke
yetu kuongoza magari haya 108 na watalii waliokuwemo bila msaada wao," aliongeza Bi. Mwangomo.
Mbali na kundi hilo la watalii 750 kutoka TUGHE, hifadhi
hiyo pia imepokea watalii wengine wa ndani 100 kutoka TASAF na 40 wa kampuni ya
UNAFRICATE.
Na. Jacob Kasiri - Tarangire
0 Maoni