DC wa Ilala awataka Wajasiriamali kuchangamkia fursa BRELA

 

Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Edward Mpogolo amewataka wafanyabiashara nchini kuchangamkia fursa kwa kurasimisha biashara zao Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) ili kunufaika na biashara wanazozifanya.       

Mhe. Mpogolo ametoa wito huo jana, alipotembelea Maonesho ya BRELA na wadau wake yanayofanyika katika uwanja wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.

Mhe. Mpogolo amesema lengo la maonesho ya BRELA ni kuhamasisha wadau kurasamisha biashara zao  kwa wingi hasa kipindi hiki ambacho BRELA imeandaa maonesho na kuzishirikisha    taasisi mbalimbali za Umma na kutoa huduma mahali pamoja.                          

Aidha, Mhe. Mpogolo amefafanua kuwa mfanyabiashara anaporasimisha biashara yake hutambulika na taasisi za kifedha, humwezesha  kupata zabuni mbalimbali pamoja na kuwa rasmi kisheria.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni Mhe. Halima Bulembo ameipongeza BRELA kwa kuandaa Maonesho yenye tija kwa wafanyabiashara na kwa ukuaji wa  uchumi nchi.

“Nimefurahishwa sana na huduma nzuri inayotolewa na BRELA, hivyo basi wafanyabiashara ambao bado hawajarasimisha biashara zao ni vyema wakafuata taratibu sahihi za kusajili,” amesema Mhe. Bulembo.

Maonesho haya ya siku tano (5) ya BRELA na Wadau wake yenye Kauli Mbiu "Urasimishaji biashara katika Mapinduzi ya  Nne ya Viwanda” yalifunguliwa Oktoba 24, 2023 na yatahitimishwa Oktoba 27, 2023 Sambamba na Mkutano wa BRELA na Wadau wake utakaofanyika katika ukumbi wa  Mlimani City Jijini Dar es Salaam.

Chapisha Maoni

0 Maoni