Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Komredi Daniel
Godfrey Chongolo amesema CCM iko salama na imara katika kusimamia misingi,
shabaha na malengo yake, ikiwemo kuendelea kuwa daraja la kusikiliza na kutatua
changamoto za wananchi.
Amesema kuwa hali hiyo inatokana na jinsi ambavyo CCM
kinaendelea kuwatumikia wananchi kwa kuzisimamia Serikali zote mbili, Serikali
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chini ya Rais Dokta Samia Suluhu Hassan na
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, chini ya
Rais Dokta Hussein Ali Mwinyi, ambazo zimeendelea kutafsiri maelekezo ya
utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020-2025, kwa vitendo.
Ndugu Chongolo amesema hayo jana , alipokutana na Katibu wa
Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Itikadi na Uenezi, Ndugu Paul Christian Makonda
na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa
(SUKI), Ndugu Rabia Abdallah Hamid, walipofika ofisini kwake, Ofisi Ndogo ya
Makao Makuu ya CCM, Mtaa wa Lumumba, jijini Dar Es Salaam, kwa ajili ya kuonana
naye, kujitambulisha na kuanza kazi, baada ya kukabidhiwa ofisi zao rasmi na
watangulizi wao.
Ndugu Chongolo aliwaelekeza
Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Itikadi na Uenezi Ndugu Paul
Makonda na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Siasa na Uhusiano wa
Kimataifa, Rabia Abdallah Hamid, kuanza majukumu yao, wakitambua imani kubwa
waliyopewa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, chini ya Mwenyekiti wa CCM, Ndugu
Dokta Samia Suluhu Hassan, kutumikia Chama kupitia nafasi hizo walizoteuliwa.
Katibu Mkuu wa CCM Ndugu Chongolo amesema kuwa nafasi hizo
mbili, Idara ya Itikadi na Uenezi na Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa,
ni mojawapo ya maeneo ya kimkakati ya CCM, hivyo wanapaswa kujua kuteuliwa kwao
ni sehemu ya kuongeza chachu na kasi ya idara hizo kutekeleza malengo
yaliyokusudiwa na CCM, katika kutumikia wananchi na kuzisimamia Serikali zote
mbili za CCM.
“Karibuni sana. Hongereni sana kwa kuaminiwa na kuteuliwa.
Ujio wenu utakuwa sehemu ya kuongeza kasi ya yale ambayo Chama tumekusudia.
Uenezi na siasa ndiyo kila kitu. Mmeaminiwa na kuteuliwa kushika maeneo muhimu".
“Siasa (na Uhusiano wa Kimataifa) ni mojawapo ya core
activities za Chama chetu. Kwa upande wa Itikadi na Uenezi ni core activity ya
siasa yetu na imani ya Chama chetu. Hatuna mashaka na ninyi. Tunatarajia
mtafanya makubwa kufikia malengo. Tuna maandalizi ya uchaguzi hapa, 2024 na
2025 (Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu). Tuko kwenye reli…tuko
kwenye track sahihi. Karibuni sana.”
Katibu Mkuu wa CCM Ndugu Chongolo, pia alitumia nafasi hiyo
kuwatakia kila la heri katika majukumu yao na kuwaelekeza kuwa, baada ya
kukabidhiwa ofisi zao na majukumu yao rasmi na watangulizi wao, waanze kazi
mara moja, kwa kuwa hakuna muda wa kusubiria.
“Najua watu wetu wa Dar Es Salaam wamewaandalia mapokezi.
Nawatakia mapokezi mema na kila la heri mnapoenda kuanza majukumu yenu rasmi.
Na Gavu (Mkuu wa Idara ya Oganaizesheni, Issa Haji Usi Gavu) atawasindikiza,”
amesema Katibu Mkuu Chongolo.
Ndugu Makonda na Ndugu Hamid, waliteuliwa kushika nafasi
hizo, hivi karibuni na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), iliyoketi katika
kikao chake maalum chini ya Mwenyekiti wa CCM, Ndugu Dokta Samia Suluhu Hassan
ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Oktoba 22, 2023, jijini
Dodoma.
Ndugu Paul Makonda aliteuliwa kuwa Katibu wa Halmashauri Kuu
ya CCM Taifa, Itikadi na Uenezi, akichukua nafasi ya Ndugu Sophia Edward Mjema
aliyeteuliwa kuwa Mshauri Ofisi ya Rais, Masuala ya Wanawake na Makundi Maalum,
ambapo Ndugu Rabia Abdallah Hamid aliteuliwa kuwa Katibu wa Halmashauri Kuu ya
CCM Taifa, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI), akichukua nafasi ya Mhe.
Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk ambaye ni Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
0 Maoni