Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa amezindua mashine ya
kuchanganya virutubisho kwenye vyakula na kuwaomba wadau wote wa maendeleo
kuunga mkono juhudi hizo ili kuwezesha mashine hizo kuzalishwa kwa wingi
kutumika katika maeneo yote hapa nchini.
Mashine iliyozinduliwa inatumika kuongeza virutubisho muhimu
katika vyakula hususan unga wa mahindi, virutubisho hivyo ni pamoja na vitamin
B na folic acid ambayo zinasaidia kwenye ukuaji wa watoto na kuzia kuzaliwa na
changamoto za ulemavu ikiwemo mgongo wazi na vichwa vikubwa.
Waziri Mkuu amezindua mashine hiyo wakati akitembelea
mabanda ya maonesho kabla ya kufunga Mkutano Mkuu wa Tisa wa Wadau wa Lishe
nchini uliofanyika katika Hoteli ya Mount Meru Jijini Arusha. “Ninawapongeza
sana wote waliowezesha kufikia hatua hii sambamba na mchango wa Shirika la
GAIN, SIDO na DIT kwa kuwezesha kazi hii kukamilika.”
Mhe. Majaliwa ametumia fursa hiyo kuwasisitiza wadau hao
wahakikishe virutubisho vinavyotumika katika mashine hizo vinazalishwa nchini
ili kuondokana na utegemezi wa kuviagiza kutoka nje ya nchi.
Aidha, Waziri Mkuu amewahakikishia wadau hao kuwa Serikali
ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan siku
zote itaendelea kuunga mkono juhudi hizi ili kuhakikisha zinakuwa endelevu.
Kadhalika Waziri Mkuu amesisitza Ofisi ya Rais - TAMISEMI
ihakikishe kuwa mikataba ya lishe kati ya Mheshimiwa Rais na Wakuu wa Mikoa
inatekelezwa kikamilifu na kuwa na tija. “Fanyeni ufuatiliaji wa karibu na
kutoa taarifa za utekelezaji mara kwa mara.”
“Watendaji Wakuu wote wa Wizara, Idara zinazojitegemea,
Wakala na Taasisi za Umma na Binafsi pamoja na Wadau wa Maendeleo na Asasi za
Kijamii wekeni malengo ya lishe katika mipango yenu pamoja na kutenga fedha za
utekelezaji kila mwaka kwa mujibu wa viwango tulivyojiwekea.”
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera,
Bunge na Uratibu, Jenista Mhagama amesema kwa kipindi kirefu nchi imekuwa
ikikabiliana na changamoto ya upatikanaji wa vifaa vya kuchanganyia virutubisho
kwenye vyakula vyenye bei nafuu, hivyo ameishukuru shirika la GAIN kwa
kuwezesha upatikanaji wa vifaa hivyo.
“Serikali imepata
mafanikio makubwa hayo kupitia Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO) na
Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam kwa kushirikiana na Shirika la GAIN
ambalo limewezesha kukamilika kwa kazi hiyo na kuwa wa kwanza kununua na
kusambaza mashine hizo katika maeneo tofauti 50 yenye wazalishaji wadogo ambao
ndio kundi kubwa linalolisha wananchi wengi.”
Awali, Naibu Waziri wa Nchi OR-TAMISEMI, Deogratius Ndejembi
alisema TAMISEMI itaendelea kusimamia utekelezaji wa huduma za afua za lishe
kwa wakuu wa mikoa pamoja na viongozi wa Mamlaka za Seikali za Mitaa kama
ilivyoainishwa katika mikataba.
Lengo kuu la Mkutano huo ni kupokea tathmini ya utekelezaji
wa masuala ya lishe nchini kwa mwaka uliopita na kutoa fursa nyingine kwa wadau
wa lishe kukutana na kupata maelezo ya tathmini ya utekelezaji wa masuala ya
lishe katika mwaka wa pili wa utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa Pili wa Kitaifa
wa Lishe (2021/22 - 2025/26) ambao ulizinduliwa mwaka 2021 Mkoani Tanga.
0 Maoni