Kongamano la Kimataifa la Sita la Magonjwa ya Ini Barani
Afrika (COLDA) limezinduliwa jijini Dar es Salaam ambapo limekutanisha
wataalamu wa magonjwa ya mfumo wa chakula na Ini, kutoka katika nchi 43 kwa
lengo la kujadili na kubadilishana uzoefu kuhusu namna ya kukabiliana na kutibu
magonjwa ya mfumo wa chakula na Ini.
Akizindua kongamano hilo kwa niaba ya Waziri wa Afya,
Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya Prof. Pascal Lugajo amesema kuwa ni heshima
kubwa kama nchi kuwa mwenyeji wa kongamano hilo kubwa ambalo limekutanisha
wataalamu wa kada mbalimbali ikiwemo Wataalamu wa Uchunguzi, Radilojia,
Wapasuaji, Wataalamu wa Mionzi na dawa.
"Magonjwa ya Ini barani Afrika na duniani kwa ujumla
yanaongezeka kwa kasi, ambapo Tanzania inakadiriwa kuwa kati ya watu 100 basi
watu 4 Hadi 8 wanamaambukizi wa homa ya Ini," amesema Prof. Lugajo
Amesema wizara ya afya inaandaa sera ya kukabili magonjwa
mbalimbali inayojumisha Magonjwa ya VVU, Magonjwa ya ngono na Hepatitis B.
"Serikali imejipanga kukabiliana na magonjwa ya Ini kwa
kufanya uwekezaji mkubwa wa vifaa vya uchunguzi na tayari wataalamu kadhaa wa
magonjwa ya homa ya ini wamepatiwa mafunzo nje ya nchi," ameeleza Prof.
Lugajo
Aidha, ametoa wito kwa wananchi kufanya uchunguzi wa
magonjwa ya Ini na kupata chanjo.
Kwa Upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa
Muhimbili Prof. Mohamed Janabi amesema kuwa MNH ni kituo kimojawapo cha
kushughulikia matatizo ya Ini na Mfumo wa Chakula kati ya vituo vinne vilivyopo
Afrika, vituo vingine vipo Morocco, Misri na Afrika kusini na kwamba tayari
kituo hicho kina wataalamu wenye weledi wa kutibu changamoto mbalimbali za
magonjwa hayo.
Kongamano la COLDA linafanyika nchini kwa siku tatu ambapo
awali lilitanguliwa na mafunzo ya kutibu magonjwa ya Ini na Mfumo wa Chakula
kwa kutumia matundu madogo.
0 Maoni