Hatukuruhusu mikutano ya hadhara ili watu wavunje Sheria- Rais Samia

 

Rais wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, amevikumbusha vyama vya siasa nchini kuwa Serikali ya awamu ya sita imeruhusu vyama vya siasa kufanya mikutano ya hadhara kwa nia ya vyama hivyo vizungumzie sera zao, mipango yao ili vyama vikue na virudishe wanachama waliopoteza.

Rais Samia ameyasema hayo leo Jijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza kwenye Mkutano wa Baraza la Vyama vya Siasa na Wadau wa Demokrasia, na kuvisihi vyama vya siasa kutumia fursa hiyo kwa kunzigatia sheria za nchi, mila na desturi zetu.

“Tumeruhusu mikutano ili vyama vikue na virudishe wale waliowapoteza, hatukutoa fursa ili watu wakavunje sheria, watu wakasimame kutukana, watu wakasimame kukashifu, watu wakasimame kuchambua dini za watu, “alisema Rais Samia na kuongeza “Lakini sishangai kwanini haya yanatokea kwa sababu yakuzungumzwa hakuna, hakuna…hakuna tulianza ooh na Katiba tukaenda ikakatika katikati, bandari imeenda sasa Katiba tena, hakuna unapokuwa hakuna cha kusema utalazimisha kunzungumza yasiyokuwepo”.

Rais Samia ameviomba vyama vya siasa nchini kwenda kutumia fursa ya mikutano ya hadhara kujijenga kwa wananchi, waelezee sera zao, kuelezea watafanya vipi na wamejipanga vipi ili wananchi warudi wawaunge mkono na watakapo ingia kwenye uchaguzi vyama vyote viwe vimesimama vizuri.

Kuhusu Katiba mpya, Rais Samia amevitaka vyama vya siasa kutouteka mchakato wa Katiba mpya na kuwaeleza wazi kwamba Katiba si mali ya wanasiasa bali ni mali ya Watanzania wote hivyo matengenezo yake yanahitaji kazi kubwa.

“Viongozi wa kisiasa tunadhani kwamba tunayo haki ya kuburuza watu tunachotaka kwenye Katiba ndio kitakua, hapana Katiba ni ya Watanzania na inahitaji kueleweka na kila mtu ili iwe rahisi kutekelezeka kwa vitendo,” alisema Rais Samia.

Ameongeza kuwa katika kufanikisha Katiba mpya, viongozi wa siasa watatoa maoni yao kwa Kamati itakayoanzisha mchakato wa Katiba mpa, na watakuwa na wawakilishi wao lakini si kila mtu atakuwepo kwenye Kamati hiyo.

Mkutano huo wa siku tatu, wenye kauli mbiu ya " Imarisha Demokrasia, Tunza Amani", umeitishwa na Msajili wa Vyama vya Siasa kwa ajili ya kuyafanyia tathimini ya mambo yaliyoinishwa na Kikosi Kazi cha Rais kilichoratibu maoni ya wadau wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa nchini.


Chapisha Maoni

0 Maoni